Swali mwigo katika tamthilia ya ‘Bembea ya Maisha’
MASKINI mke wangu! Kumbe ugonjwa haukumsaza mwaka baada ya mwaka.
Umemla bila huruma. Awali niliona kama mchezo. Kumbe ilikuwa kweli! Kauli yake ninaona imesimama.
Ni mwele hakika. Laiti ningejua, jana ningeishi tofauti. Silesi zetu za maisha tungezila zilivyokuja kwa furaha. Siku hazigandi wala jana haitarudi.
Sasa jana imebaki kuwa kumbukizi baada ya kusombwa na wakati mfano wa mafuriko msimu wa masika.
Kwa bahati nzuri bado tupo. Ninaweza kuiachia dunia tabasamu iwe silesi kwa vizazi vijavyo na kila mwenye nia njema.
Siwezi kuendelea kuishi hivi. Sasa nimekata shauri.
Lazima niache njia ya zamani na kuifuata mpya. Maisha mapya. Pombe! Umenichezesha kama mwanasesere kwa muda mrefu.
Umeninyima fursa ya kuielewa familia yangu. Hapana! Siku zangu za uzeeni lazima nizitumie kumwangalia mke wangu mgonjwa.
Lazima nimshukuru kwa vitendo kwa jinsi alivyojitolea kuijenga familia yetu. Kwaheri pombe. Buriani.
a) Changanua mitindo minane katika kifungu hiki.
Nidaa – maskini mke wangu! Kumbe ilikuwa kweli!
Mbinu rejeshi – Awali niliona kama mchezo. Kumbe ilikuwa kweli!
Utohozi – silesi zetu za maisha- (slices of life).
Tashibihi – Umenichezesha kama mwanasesere kwa muda mrefu.
Tashihisi – Kauli yake ninaona imesimama. Ugonjwa umemla bila huruma, pombe umenichezesha kama mwanasesere kwa muda mrefu.
Ritifaa – Kwaheri pombe. Buriani.
Uzungumzi nafsia – kifungu chote Yona anajisemea.
Istiara – Silesi zetu za maisha tungezila zilivyokuja kwa furaha akirejelea matatizo ya maisha.
Nahau – Sasa nimekata shauri.
b) Jadili maudhui tisa yanayojitokeza katika kifungu hiki.
Majuto – Yona anajutia mienendo yake ya awali: Laiti ningejua, jana ningeishi tofauti.
Mabadiliko – Yona anaamua kuacha pombe na kutumia siku zake za uzeeni kumwangalia mkewe: Siku zangu za uzeeni lazima nizitumie kumwangalia mke wangu mgonjwa.
Ndoa – Yona anasema “Maskini mke wangu!”
Athari za ulevi – Ulevi unamnyima Yona fursa ya kulea familia yake: Umeninyima fursa ya kuielewa familia yangu.
Ugonjwa – Kumbe ugonjwa haukumsaza mwaka baada ya mwaka. Umemla bila huruma.
Mapuuza- Awali niliona kama mchezo. Kumbe ilikuwa kweli!
Matumaini- Kwa bahati nzuri bado tupo. Ninaweza kuiachia dunia tabasamu iwe silesi kwa vizazi vijavyo na kila mwenye nia njema.
Mwanzo mpya – Siwezi kuendelea kuishi hivi. Sasa nimekata shauri. Lazima niache njia ya zamani na kuifuata mpya. Maisha mapya.
Uwajibikaji – Siku zangu za uzeeni lazima nizitumie kumwangalia mke wangu mgonjwa.
Shukrani – Lazima nimshukuru kwa vitendo kwa jinsi alivyojitolea kuijenga familia yetu.
c) Tambua toni tatu zinazojitokeza katika kifungu hiki
Toni ya huzuni – Maskini mke wangu! Kumbe ugonjwa haukumsaza mwaka baada ya mwaka.
Toni ya majuto – Yona anajutia matendo yake ya kumpuuza mkewe (Sara) mgonjwa. Ni mwele hakika. Laiti ningejua, jana ningeishi tofauti.
Toni ya matumaini – Siku zangu za uzeeni lazima nizitumie kumwangalia mke wangu mgonjwa.