Maoni

MAONI: Hatari kubwa zaidi ya kuvumilia uhuni ni kwamba haramu inakuwa halali, na halali haramu

Na DOUGLAS MUTUA April 23rd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KENYA tuna tatizo kubwa – mwibuko wa magenge hatari. Tatizo lenyewe ni la kujiletea sisi wenyewe, hasa kwa sababu magenge mengi yameanzishwa na watu mashuhuri, wanasiasa, na yanaungwa mkono na Serikali.

Hali imekuwa mbaya hivi kwamba wanasiasa wanajiundia magenge hayo na kuyafadhili kikamilifu, nia ikiwa moja tu: kutishia watu kwamba matumizi ya nguvu ni mojawapo ya afua zinazoweza kuzingatiwa hali ikibidi.

Inapotukia kuwa vyombo vya kawaida vya usalama havitoshi kuwalinda wananchi, kiasi kwamba wanaishia kujiundia magenge yao wenyewe, basi nchi inaelekea pabaya. Haramu inakuwa halali, na halali inakuwa haramu.

Wote, Serikali na upinzani, wamo lawamani kwa kuwa tumewahi kushuhudia magenge yenye silaha hatari yakiungana na polisi kukabiliana na waandamanaji wanaopinga sera za Serikali.

Tumewahi kushuhudia, hasa wakati wa chaguzi ndogo ambazo zilifanyika sehemu mbalimbali nchini hivi majuzi, watu wakipigwa, kuvuliwa nguo na kuachwa uchi wa mnyama!

Pia tumeshuhudia watu wakipigilia misumari kwenye mipini na kuitumia kutoboa magurudumu ya magari ya mahasidi wao wa kisiasa, na vilevile kuwapiga wanasiasa hao kwa silaha nyingine duni ila hatari. Kuvaa kofia za kukinga vichwa ukihudhuria mikutano ya hadhara si mzaha tena, ni hitaji la kimsingi.

Tumewaona wahalifu wakishirikiana na polisi kuwashambulia wanasiasa wa upinzani kwenye makanisa na mikutano ya hadhara, wala hakuna hatua wanazochukuliwa kwa kuwa uhalifu wao unatakaswa na kufumbiwa macho na Serikali.

Kenya imekuwa kioja. Tulifikaje huko kwa polisi kushirikiana sako kwa bako na wahalifu, kuwadhuru wananchi? Hiyo ndiyo ishara ya kwanza kwamba taifa linakaribia kufeli. Kuna hakika gani kwamba polisi hawawezi kuyapa magenge hayo silaha ili yakamilishe kazi hiyo ya kihalifu?

Wanasiasa binafsi nao wanatembea huku na kule chini ya ulinzi mkali wa watu wanaojifanya walinzi rasmi ilhali hawana mafunzo yoyote, wala hawatambuliwi kisheria. Kinachowapa fursa za kuwa walinzi wa ‘waheshimiwa’ ni uwezo wa kutumia nguvu kupitiliza, sikwambii na kukaza sura.

Magenge hayo yakivunja sheria, watetezi wake wakuu ni wanasaisa, kama inavyoshuhudiwa mjini Kitale, ambako Waziri wa Usalama wa Ndani, Bw Kipchumba Murkomen, anabishana na Gavana wa Trans-Nzoia, Bw George Natembeya, kuhusu hatua ya Serikali kuyakabili magenge.

Waziri wa watu anasema vijana waliojiunga na magenge hayo yapondwe kisawasawa, naye Gavana Natembeya anasisitiza kuwa kutumia nguvu dhidi ya vijana hao ni kukiuka haki zao za kimsingi.

Ukweli usemwe japo unauma; Serikali haina uhuru wa kuua mtu yeyote bila kumpitishia kwenye mchakato mzima wa sheria, yaani kushtakiwa, kusikiziwa kesi, kuhukumiwa na hatimaye kuadhimiwa iwapo hatia itapatikana.

Serikali inapowaumiza raia au kuwaua, bila kufuata mchakato huu, basi huko ndiko kunakoitwa kuvunja haki za kimsingi za binadamu na inaweza kushtakiwa kwa kukiuka Katiba ya nchi.

Vile vile, mtu yeyote, awe gavana au la, hana uhuru wa kuunda genge lolote linalotenda kazi nje ya utaratibu wa sheria za nchi. Kufanya hivyo ni kushiriki uhalifu; lolote linalotendwa na kundi husika, mwanzilishi analaumiwa kwa njia ya haki. Likiua watu, damu yao iko juu ya mwanzilishi.

Mataifa yaliyofeli yakadhibitiwa na magenge hatari huanzia kwa kuuona uhalifu huo kama kitu cha kawaida, yaani hali ikawa ya mwenye nguvu mpishe, lau sivyo uvunjwe mbavu bure.

Magenge nchini Haiti yaliigawa nchi yao vigae huku dunia ikitizama tu na kupuuza, mwishowe ikawa dharura ya kushughulikiwa na kila mtu.

Kenya, na hapa narejelea Serikali na wadau wengine wanaotumia magenge, haipaswi kusubiri hadi utovu wa usalama uwe janga la kitaifa, suluhisho linahitajika leo.

Wadau wanapaswa kuonyesha uzalendo kwa kuitakia nchi yao mema matupu, badala ya kuidhuru, hasa wakati huu ambapo tunaendelea kukaribia uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.

Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika (mutua_muema@yahoo.com)