Wakulima wahimizwa kuepuka pembejeo feki za kilimo
Kwa mara nyingine tena wakulima katika eneo la Nyanza wamepokea hamasisho kuhusu namna ya kukabiliana na pembejeo feki.
Hatua hii inalenga kuwaepusha na hasara zinazotokana na ununuzi wa bidhaa ghushi kama vile mbolea na mbegu.
Hamasisho hilo lililoandaliwa mjini Kisii Jumatano, Aprili 22 na kuwaleta pamoja wakulima kutoka kaunti za Kisii na Nyamira.
Mashirika mbali mbali yanayoongoza vita hivyo yakiwemo Bayer East Africa na kampuni ya mbegu ya Dekalb yaliwataka wakulima kuwa makini wanaponunua pembejeo hizi ili kuepuka kupunjwa na madalali wanafiki.
Afisa wa Bayer East Africa Barnabas Moseki alidokeza kuwa Kenya ni miongoni mwa mataifa ambayo kero la kughushiwa kwa bidhaa kama vile pembejeo lilikuwa limekithiri.
Bw Moseki aliwataka wakulima kununua mbegu na pembejeo zingine kutoka kwa maduka na maajenti ambao wameidhinishwa na asasi muhimu za serikali kama vile Shirika la Kephis, ambalo linahusika na afya ya mimea.”Wakulima wanafaa wawe macho wasiuziwe pembejeo feki msimu huu. Ndiyo maana tumekuja kuwaeleza wakulima kuhusu mpango huo,” Bw Moseki alisema.
Alionya kuwa mbegu ghushi ni tishio kubwa la kiuchumi, kwani wakulima mara nyingi hutumia pesa zao walizochuma kwa bidii kwa mbegu ambazo zinashindwa kutoa mavuno yanayotarajiwa.
“Mkulima anaponunua mbegu ambayo haifanyi kazi, inaleta tija ndogo na hasara ya kifedha. Mbegu halisi zilizoidhinishwa huhakikisha viwango vya juu vya kuota na utendakazi bora,” Bw Moseki aliongeza.
Katika hamasisho hilo, mkulima mmoja Richard Atambo kutoka kaunti ya Nyamira alijishindia pikipiki kutoka kwa kampuni ya Dekalb.