IEBC yawazia kuzuia wafungwa kuchagua rais
Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) inawazia mabadiliko makubwa ya sera yatakayoruhusu wafungwa kupiga kura kuchagua wawakilishi katika viti vyote vitano vya uongozi isipokuwa urais, katika hatua inayolenga kuongeza ushirikishaji wa kidemokrasia nchini.
Kwa sasa, wafungwa nchini Kenya wanaruhusiwa kupiga kura kuchagua Rais pekee. Hata hivyo, pendekezo jipya likipitishwa, wafungwa wataweza kwa mara ya kwanza kushiriki uchaguzi wa Gavana, Seneta, Mwakilishi wa Wanawake, Mbunge na Mwakilishi wa Wadi.
Naibu Mwenyekiti wa IEBC Fahima Araphat alisema tume imeweka mikakati maalum ya kuhakikisha kila Mkenya anayestahili anapata nafasi ya kujisajili kama mpiga kura, bila kujali mahali alipo, wakiwemo wafungwa walioko magerezani.
Alisema IEBC inapanga kubadilisha magereza kuwa vituo rasmi vya kupigia kura, hatua itakayosaidia kuhakikisha usawa na uwazi katika mchakato wa uchaguzi.
“Hatutaki kubagua yeyote. Wafungwa wana haki ya kikatiba kushiriki uchaguzi, na tutaweka mifumo itakayohakikisha wanapata nafasi hiyo,” alisema wakati wa ziara yake Taita Taveta.
Aliongeza kuwa tume pia inafikiria kuruhusu maafisa wa magereza pamoja na familia zao kupiga kura katika vituo hivyo vya magereza, ili kuongeza ufanisi wa mchakato wa uchaguzi.
Kwa mujibu wa Katiba ya Kenya, kila raia mtu mzima mwenye akili timamu na ambaye hajapatikana na hatia ya makosa ya uchaguzi ndani ya kipindi cha miaka mitano ana haki ya kupiga kura. Hii ina maana kuwa wafungwa wengi, hasa wale waliopatikana na hatia kwa makosa yasiyo ya uchaguzi, wanastahili kushiriki uchaguzi.
Mahakama pia iliwahi kuunga mkono haki hii katika kesi ya 2013 ya Kituo Cha Sheria dhidi ya IEBC, ambapo ilibainisha kuwa hakuna sheria inayowanyima wafungwa wanaokidhi vigezo vya kikatiba kushiriki uchaguzi. Uamuzi huo ulisisitiza kuwa demokrasia haiwezi kuwa kamili iwapo baadhi ya wananchi wanaondolewa bila msingi wa kisheria.
Wakati huo huo, IEBC imeongeza kasi ya usajili wa wapiga kura kote nchini katika zoezi ambalo linatarajiwa kufungwa Aprili 28 2026. Tume inalenga kusajili zaidi ya wapiga kura milioni 2.5 wapya, na tayari zaidi ya milioni 1.3 wamesajiliwa.
Kamishna wa IEBC Francis Aduol aliwahimiza vijana kujitokeza kwa wingi kujisajili kama wapiga kura, akisema kuwa kundi hilo lina nguvu kubwa ya kuamua mustakabali wa uongozi wa nchi.