Papa akemea maaskofu Ujerumani kuhusu kubariki ndoa za jinsia moja
KIONGOZI wa Kanisa Katoliki duniani, Papa Leo XIV, amewakemea hadharani maaskofu wa Ujerumani kufuatia mwongozo unaoruhusu wanandoa wa jinsia moja kupokea baraka za kanisa, akisisitiza kuwa hatua hiyo inakiuka msimamo rasmi wa Vatican kuhusu ndoa.
Akizungumza akiwa njiani kurejea Vatican baada ya ziara ya siku kadhaa barani Afrika, Papa Leo alisema uongozi wa Kanisa tayari ulikuwa umeweka wazi kutoridhishwa kwake na hatua ya baadhi ya maaskofu wa Ujerumani kutoa baraka hizo.
“Kanisa limezungumza na maaskofu wa Ujerumani na limeweka wazi kuwa halikubaliani na baraka rasmi kwa wanandoa wa jinsia moja au mahusiano yaliyo nje ya mafundisho ya kawaida ya ndoa,” alisema Papa huyo.
Kauli hiyo imejiri siku chache baada ya Askofu Mkuu wa Munich na Freising, Kardinali Reinhard Marx, kuidhinisha baraka kwa wanandoa wa jinsia moja katika dayosisi yake, hatua iliyochochewa na mwongozo wa pamoja wa Jumuiya ya Maaskofu wa Ujerumani na Kamati Kuu ya Wakatoliki nchini humo.
Papa Leo, anayechukuliwa kuwa mwenye msimamo wa kihafidhina zaidi kuhusu masuala ya kijamii, alisisitiza kuwa umoja wa kanisa haupaswi kutikiswa na mijadala ya masuala ya ngono.
“Umoja au mgawanyiko wa Kanisa haupaswi kuzunguka suala hili pekee. Kuna masuala makubwa zaidi kama haki, usawa, uhuru wa dini na hadhi ya binadamu yanayostahili kupewa uzito,” alisema.
Msimamo wake unaonekana kukinzana na mtazamo wa marehemu Papa Francis, ambaye wakati wa uongozi wake alionekana kulegeza kamba kuhusu makundi ya LGBTQ, ingawa hakuwahi kubadili mafundisho rasmi ya Kanisa kuhusu ndoa kuwa kati ya mwanaume na mwanamke.
Mwaka 2023, chini ya Papa Francis, Vatican kupitia waraka Fiducia Supplicans iliruhusu mapadri kutoa baraka zisizo rasmi kwa watu walio katika mahusiano ambayo hayalingani na mafundisho ya Kanisa, ikiwemo wanandoa wa jinsia moja, mradi baraka hizo zisiwe sehemu ya ibada ya ndoa au kuonekana kama kuhalalisha muungano huo.
Hatua hiyo ilizua mjadala mkali ndani ya Kanisa, huku baadhi ya maaskofu hasa Ulaya wakiiunga mkono, lakini wengine hasa Afrika na sehemu za Asia wakipinga wakisema ilizua mkanganyiko wa mafundisho.
Papa Francis pia aliwahi kuvutia hisia za wengi aliposema, “Mimi ni nani nihukumu?” akirejelea waumini mashoga wanaomtafuta Mungu, kauli iliyotafsiriwa kama ishara ya huruma lakini si mabadiliko ya mafundisho.
Sasa Papa Leo anaonekana kuchukua msimamo dhabiti akionya kuwa tafsiri zinazoweza kuonekana kupanua maana ya ndoa ya Kikristo zinaweza kuleta mgawanyiko katika Kanisa.
Mvutano huu unaendelea kuonyesha mgongano unaokua ndani ya Kanisa Katoliki kati ya msukumo wa mageuzi katika baadhi ya maeneo, na msisitizo wa kuhifadhi mafundisho ya jadi kutoka Vatican.