Habari za Kitaifa

Ruto amlima Gachagua akimrejelea kama dikteta

Na DAVID MUCHUI April 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto jana aliendelea kumshambulia aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, akimshutumu kwa kukandamiza haki na uhuru wa kidemokrasia wa wakazi wa Mlima Kenya.

Kiongozi wa nchi alimkosoa Bw Gachagua, huku akimrejelea kama dikteta, akisema ni “mbaya zaidi kuliko wakoloni na wafanyabiashara wa watumwa.”

Alisisitiza kuwa hatasalimu amri kwa shinikizo la kisiasa kutoka kwa kiongozi huyo wa DCP akimtuhumu kujaribu kudhibiti sehemu za nchi.

Akizungumza katika Chuo cha Walimu cha Rubate, Kaunti ya Tharaka-Nithi, Dkt Ruto aliwataka Wakenya kuwachagua viongozi kulingana na rekodi yao ya maendeleo, badala ya semi tatanishi za kisiasa.

Aliandamana na Profesa Kindiki, Gavana wa Tharaka-Nithi Muthomi Njuki, Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru mwenzake wa Embu Cecily Mbarire na Waziri wa Ardhi Alice Wahome miongoni mwa viongozi wengine.

“Kuna viongozi wanaodhani wanajua kila kitu na wanaweza kudhibiti maisha yetu. Zamani tulikuwa na wafanyabiashara wa watumwa na wakoloni, lakini walikuwa na kiasi fulani cha kujizuia. Baadhi ya viongozi wa leo wamewazidi,” akasema Rais Ruto.

Alisisitiza kuwa anafanya kazi ya kuunganisha taifa kueneza maendeleo maeneo yote bila kujali iwapo wakazi wake walimpigia kura au la.

“Alitaka kudhibiti sana lakini tulimkataa. Eti yeye ndiye angeamua nani akutane na nani, nani aende Ikulu, hata kile mnakula na kunywa. Usipofuata, unaitwa msaliti. Amewazidi hata wafanyabiashara wa watumwa na wakoloni,” akaongeza Rais Ruto.

Rais alisisitiza kuwa hakuna mtu atakayemzuia kutekeleza majukumu yake mahala popote nchini.

“Amevuka mipika hadi kudai nipige magoti mbele yake lakini mimi hupiga magoti mbele ya Mungu pekee. Nawahakikishia watu wa Mlima Kenya kuwa hakutakuwa na mabwana wa watumwa nchini Kenya na hakuna anayeweza kuchukua mamlaka ya wananchi,” alisema.

Kuhusu Profesa Kindiki, Dkt Ruto alisema Profesa Kindiki ni mchapakazi na hata amezidi uwajibikaji wake alipokuwa akihudumu chini ya Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta.

“Hatuwezi kupata naibu rais bora kuliko Profesa Kithure Kindiki. Hana kiburi. Katika muda mfupi tuliokuwa tumefanya kazi pamoja, amefanya vizuri zaidi kuliko nilivyofanya nikiwa naibu rais,” alisema.

Kwa upande wake, Profesa Kindiki alimshutumu mtangulizi wake kwa kujitangaza kama kinara wa eneo bila kuonyesha matokeo halisi.

“Hujitangazi kuwa kinara kwa sababu kazi yako ndiyo hukupa heshima. Eneo hili limetoa marais watatu, lakini hakuna aliyekuwa akizunguka akijitangaza mfalme wa mlima. Simba haitangazi usimba wake,” akasema Profesa Kindiki.

Aliongeza kuwa swali la nani ataongoza Mlima Kenya litaamuliwa na wapiga kura katika uchaguzi wa 2027.

Rais Ruto pia aliwapuuzilia mbali wapinzani wake akisema hawana rekodi ya utendaji bali wamejaa matusi na kiburi.