Habari

Mswada unaolenga kuwazuia magavana kuwania ubunge na udiwani, wawasilishwa mbele ya Bunge la Seneti

Na SAMWEL OWINO April 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAGAVANA watazuiwa kugombea viti vya ubunge au udiwani kwa kipindi cha miaka mitano iwapo Mswada unaotathminiwa kwa sasa mbele ya Bunge la Seneti utapitishwa.
Mswada wa Marekebisho ya Katiba ya Kenya, 2026, ambao umedhaminiwa na Seneta wa Kirinyaga James Murango, unalenga kuwazuia magavana waliomaliza muhula wao kuwania ubunge au udiwani ili kuzuia mgongano wa maslahi katika taasisi za kikatiba zimepewa jukumu la kuwasimamia.
Sheria inayopendekezwa inalenga kurekebisha Katiba kuwafungia magavana kuwania viti vya ubunge na uwakilishi wadi.
“Lengo la pendekezo hili la kisheria ni kuwazuia watu waliowahi kuhudumu kama magavana kuwania ubunge au mwakilishi wadi kwa kipindi cha kwanza cha miaka mitano mara tu baada ya kuondoka madarakani,” inasema mswada huo.
Bw Murango anahoji kuwa kuwazuia magavana wa zamani kugombea kutaruhusu michakato inayoendelea ya ukaguzi wa fedha kutoingiliwa na wanasiasa wanaoshikilia nyadhifa hizo mbili.
“Kwa kuwa Seneti na mabunge ya kaunti yanatekeleza jukumu la usimamizi wa serikali za kaunti kwa kudadavua wa ripoti za ukaguzi na kuwawajibisha magavana kuhusu uongozi wao, kuruhusu magavana wa zamani kuketi katika mabunge haya kutasababisha mgongano wa majukumu na kuathiri ukaguzi wa matumizi ya fedha,” ikaongeza mswada huo.
Seneta huyo anasema kipindi hicho cha miaka mitano kitawapa taasisi za usimamizi muda wa kutosha kutekeleza majukumu yao bila kuingiliwa.
“Taasisi za usimamizi zitakuwa na muda wa kutosha kuchunguza masuala yoyote yanayotokana na kipindi cha uongozi wa gavana wa zamani bila kuingiliwa,”
Aidha, anasema kipindi hicho kitawapa wapigakura nafasi ya kufanya maamuzi kuhusu uliokuwa uongozi wa magavana kabla ya kuwachagua kushikilia nyadhifa nyingine.
“Kuwazuia magavana wa zamani kugombea kutawapa raia muda wa kutosha kujua jinsi walivyotumia fedha na muda wa kutatuliwa kwa masuala hayo,”
Katika utekelezaji wa majukumu yao, magavana wa kaunti wanatakiwa kuwajibika mbele ya mabunge ya kaunti na Seneti kuhusu matumizi ya fedha za kaunti.
Ripoti za kila mwaka za ukaguzi zinazoandaliwa na Afisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali huwasilishwa kwa Seneti na mabunge husika ya kaunti kwa uchunguzi.
Wasiwasi ni kwamba iwapo gavana atachaguliwa kama seneta anaweza kuhitilafiana na uchunguzi na pia itakuwa vigumu kwake kuchunguzwa na seneti hiyo hiyo anakohudumu.
Katika Seneti ya sasa, Seneta wa Uasin Gishu anahudumu licha ya kuwa hapo awali alikuwa seneta wa kaunti hiyo kwa mihula miwili.