Kindiki, Waiguru na Ichung’wah kuvumisha upya ‘Tutam’ Mlimani
RAIS William Ruto amefanya mabadiliko makubwa katika mkakati na kikosi chake cha wanasiasa washirika katika eneo la Mlima Kenya, hatua inayolenga kuimarisha uungwaji mkono kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Hatua hiyo inajiri huku aliyekuwa Naibu Rais, Rigathi Gachagua, akiendelea kushambulia vikali serikali ya Kenya Kwanza katika eneo hilo lenye kura nyingi.
Katika mkakati huo mpya, Rais anategemea kikosi cha wanasiasa, wataalamu wa serikali na viongozi wa chama cha United Democratic Alliance (UDA) ili kuimarisha ushawishi wake.
Kinara wa mkakati huo ni Naibu Rais Kithure Kindiki, ambaye ameibuka kama mhimili mkuu wa juhudi za kuimarisha uungwaji mkono wa serikali katika eneo hilo.
Profesa Kindiki sasa anaongoza kile kinachotajwa kama “kikosi cha kampeni” ya Rais Mlima Kenya, akichanganya uhamasishaji wa kisiasa, ujumbe wa maendeleo ya serikali na mipango ya mawasiliano ili kurejesha imani ya wananchi.
Katika mikutano ya hadhara ya hivi karibuni, Rais Ruto amekuwa akimsifu wazi wazi Naibu wake, akionyesha imani naye na hata kuwataka wananchi kuthibitisha uungwaji mkono wao.
Kauli hiyo imechochea tetesi kuwa Profesa Kindiki huenda akawa mgombea mwenza wa Rais katika uchaguzi wa 2027.
Miongoni mwa viongozi walioko katika kikosi hicho ni Gavana wa Kirinyaga Anne Waiguru, Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung’wah na Mbunge wa Laikipia Mashariki Mwangi Kiunjuri, ambaye pia ni kiongozi wa chama cha TSP.
Wengine ni pamoja na Naibu Mkuu wa Utumishi wa Umma Amos Gathecha, mwenyekiti wa bodi ya uchaguzi ya UDA Anthony Mwaura, Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku, Waziri wa Ardhi Alice Wahome, Katibu wa Nishati Alex Wachira na Katibu wa Afya ya Umma Mary Muthoni.
Aliyekuwa Waziri wa Biashara Moses Kuria na baadaye mshauri mkuu wa uchumi, anaendelea kuwa na ushawishi mkubwa katika mikakati ya kisiasa ya Rais, hasa katika uhamasishaji wa mashinani.
Katika ngazi ya chama, Gavana wa Embu Cecily Mbarire ambaye pia ni mwenyekiti wa kitaifa wa UDA, anasimamia shughuli za chama na kuimarisha miundo ya mashinani.
Viongozi wengine wanaosaidia juhudi hizo ni Mbunge wa Mathira Eric Wamumbi, Mbunge wa kuteuliwa Sabina Chege, Mbunge wa Maragua Mary Wamaua, Mwakilishi wa Wanawake wa Murang’a Betty Maina, Seneta wa Nyeri Wahome Wamatinga, Gavana wa Tharaka Nithi Muthomi Njuki na Gavana wa Meru Mutuma M’Ethingia.
Kwa mujibu wa wachambuzi, mkakati huo unalenga kuunganisha maendeleo ya serikali na ujumbe wa kisiasa ili kuwavutia wapigakura, huku ukijibu madai ya upinzani kuwa eneo hilo limetengwa.
Katika mikutano yake, Profesa Kindiki amekuwa akisisitiza kuwa kuunga mkono muhula wa pili wa Rais Ruto mwaka 2027 kutafungua njia kwa Mlima Kenya kupata urais mwaka 2032.
“Ni rahisi kungoja miaka mitano kuliko kumi. Huo ndio mkakati wa kisiasa,” amesema katika mikutano ya hivi karibuni.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Multimedia Profesa Gitile Naituli anasema mbinu ya Naibu Rais kupunguza mashambulizi dhidi ya Gachagua ni ya kimkakati, ingawa huenda isitoshe kubadili hisia za wapigakura.
Hata hivyo, kivuli cha Rigathi Gachagua kinaendelea kutanda katika eneo hilo, akiwa amejitangaza kama mtetezi wa maslahi ya Mlima Kenya na kukosoa serikali kwa madai ya kupuuza eneo hilo.
Wakati huo huo, juhudi za Rais Ruto zinajiri huku kukiwa na mazungumzo ya kisiasa na Orange Democratic Movement (ODM), hatua inayoweza kubadilisha mwelekeo wa siasa za kitaifa.
Kwa sasa, mkakati wa Rais unaonekana kulenga kudumisha uungwaji mkono wa Mlima Kenya huku akipanua ushawishi wake kitaifa—mizani ambayo wachambuzi wanasema itakuwa muhimu katika safari yake ya kutetea kiti chake mwaka 2027.