Siasa

Sijawazia urais, lengo kwanza ni kujenga vuguvugu kali la kung’oa Ruto – Sifuna

Na MWANGI MUIRURI May 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SENETA wa Nairobi, Edwin Sifuna, amesema bado hajaamua atagombea wadhifa gani katika Uchaguzi Mkuu wa 2027, licha ya umaarufu anaopata kupitia mrengo wake wa Linda Mwananchi ndani ya chama cha Orange Democratic Movement (ODM).

Akizungumza jana, Bw Sifuna alisisitiza kuwa juhudi zake hazilengi maslahi yake binafsi bali ustawi wa wananchi, akiongeza kuwa anataka kujikita katika mjadala wa pamoja unaoweka wananchi mbele.

“Tulicho nacho ni wazo la maslahi ya wote, linaloungwa mkono na wananchi. Tunapaswa kuwaambia kuwa hatutawaangusha. Tunapotaka mabadiliko ya uongozi, lazima pia tutoe sababu ya kuaminika kwamba tuko tayari kuchukua nafasi hiyo,” alisema.

Alisema mwelekeo huo ndio unaomsukuma kushiriki katika juhudi za kumshinda Rais William Ruto katika uchaguzi wa 2027, akidai maoni kutoka kwa wafuasi wake yanaonyesha hamu ya “kuikomboa nchi” kutoka kwa utawala wa sasa.

Akizungumza katika kituo cha redio cha Spice FM, Bw Sifuna, aliyejitaja kama kinara wa jamii ya Abaluhya, alisema mpango wake wa kwanza ni kuzuru maeneo mbalimbali nchini pamoja na washirika wake ili kukusanya maoni ya wananchi na kuunda mkakati madhubuti wa kisiasa.

“Sifuna kuwa rais? Si kuhusu Sifuna. Kwanza tunajenga vuguvugu lenye nguvu. Tunahitaji idadi ya kutosha kushinda serikali. Masuala ya azma binafsi tutayashughulikia baadaye. Hii lazima iwe kampeni ya wananchi,” alisema.

Aliongeza kuwa mtazamo wake umechochewa na marehemu Raila Odinga, ambaye alisema alimhimiza kusimama upande wa wananchi bila woga.

“Raila alinifunza kuwa ukiwa upande wa wananchi, huna cha kuogopa. Hilo ndilo linafanya shughuli za Linda Mwananchi kufanikiwa,” alisema.

Bw Sifuna pia alidai kuwa marehemu Odinga hakuwahi kuunga mkono azma ya Rais Ruto ya kuchaguliwa tena mwaka 2027, akisema aliamini kuwa Rais huyo amedhoofika kisiasa.

Kwa mujibu wake, upinzani wake dhidi ya serikali hauchochewi na chuki bali ni kutokana na kile alichokitaja kuwa kuvunjwa kwa matarajio ya wananchi waliopiga kura mwaka 2022.

“Vijana hasa wamesema wazi wanataka serikali hii iondoke. Wanataka uhuru na utawala unaozingatia Katiba,” alisema.

Alishutumu serikali kwa kutoa ahadi zisizotekelezeka na kutumia miradi ya maendeleo vibaya.

“Maendeleo ni mazuri, lakini lazima yawe na nia njema. Hauwezi kujenga barabara ili kurahisisha utekaji wa vijana. Jenga viwanja vya michezo, lakini kwa uwazi katika zabuni. Hauwezi kuwapa vijana fedha bila kusema ni mkopo wa Benki ya Dunia,” alisema.

Aidha, alimkosoa Waziri wa Usalama wa Ndani, Bw Kipchumba Murkomen, kwa madai ya kusambaza taarifa zisizo na msingi kuhusu ufadhili wa vuguvugu lake.

Bw Sifuna alikanusha madai kwamba wanapokea fedha kutoka kwa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, akisema shughuli zao zinafadhiliwa na michango ya wanachama na wafadhili binafsi.

“Wanaodai hivyo hawajatoa ushahidi. Tunaweza kuonyesha jinsi tunavyojifadhili. Hata mkutano wa Kisumu ulifadhiliwa na wanachama na wafadhili wengine,” alisema.

Alisema wafuasi wa ODM wameungana kupinga kuchaguliwa tena kwa Rais Ruto.

“Wafuasi wote wa ODM hawataki Rais Ruto arejee madarakani. Hakukuwa na uamuzi wowote wa chama kumuunga mkono. Maoni tuliyopokea yanaonyesha wazi hawamtaki,” alisema.

Alisisitiza kuwa upinzani lazima ujibu kilio cha wananchi kwa kurejesha utawala unaozingatia uwazi, haki na uadilifu.

“Hatuwezi kuendelea na mfumo ambao unaathiri ajira na huduma za umma. Tunataka kurejesha misingi ya haki na uwajibikaji nchini,” alisema.