Habari za Kaunti

Mashambulio yazidi kuzua taharuki Kitui polisi wakikamata waandamanaji

Na DANIEL OGETTA May 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

TAHARUKI inaendelea kutanda katika mji wa Mwingi, Kaunti ya Kitui pamoja na jamii zinazoishi kando ya barabara kuu ya Mwingi–Garissa kufuatia msururu wa mashambulizi yanayodaiwa kutekelezwa na wafugaji kutoka kaunti jirani za Tana River na Garissa, hali inayotishia kuzorota zaidi.

Tangu Jumanne hadi Jumatano, shughuli za usafiri na biashara zilisimama katika barabara hiyo huku wakazi wakifanya maandamano kulalamikia mauaji ya hivi karibuni yaliyoongeza taharuki eneo hilo.

Maandamano hayo yalichochewa na mauaji ya mvulana wa miaka 14 yaliyotokea Jumanne katika eneo la Ukasi, mji wa mpakani kati ya kaunti za Kitui na Tana River.

Wakazi walitaja tukio hilo kama la kinyama na lisiloeleweka. Mauaji hayo yalifuatia mengine ambapo watu saba waliripotiwa kuuawa katika eneo la Kwa Kamari, Tseikuru, Jumamosi iliyopita, hali iliyozidisha mivutano iliyokuwepo.

Ingawa matukio hayo yalitokea mbali kutoka barabara kuu, hasira zilijitokeza katika miji iliyo kando ya barabara hiyo, huku Mwingi ikiwa kitovu cha vurugu.

“Tunataka serikali itusikie kupitia maandamano haya,” alisema Bi Christine Mueni, mfanyabiashara wa Mwingi, huku moshi wa vitoa machozi ukionekana nyuma yake.

“Tunatumaini suluhisho la kudumu litapatikana ili tusiendelee kupoteza maisha zaidi.”

Gavana wa Kitui, Bw Julius Malombe na mwenzake wa Garissa, Bw Nathif Jama, walitarajiwa kukutana jana kujadili hali ya usalama katika eneo hilo.

Sehemu mbalimbali za barabara ya Mwingi–Garissa zilifungwa kwa vizuizi katika maeneo ya Ukasi, Nguni na Mwingi, na kufanya barabara hiyo kutopitika.

Biashara nyingi zilifungwa, huku baadhi ya maduka Mwingi yakivamiwa na kuporwa.

Ghasia hizo zinahusishwa na mivutano ya muda mrefu kati ya wakulima wa Kitui na wafugaji wanaohamahama kutoka kaunti jirani.

Kiini cha mgogoro huo ni mizozo ya malisho na upatikanaji wa rasilimali, huku wakazi wakidai wafugaji wanavamia ardhi yao, ilhali wafugaji wanategemea eneo hilo kwa malisho ya mifugo.

Bw Haron Munalia, mkazi wa Mwingi, alisema mzunguko huo wa vurugu unaathiri pande zote.

“Jamii zote zinapoteza. Wafugaji huleta mifugo, na huku ndiko soko. Lakini sasa kila kitu kimesimama,” alisema.

Kupitia taarifa, Huduma ya Taifa ya Polisi ilikiri kuwepo kwa “mashambulizi ya wahalifu katika maeneo ya Tseikuru na Ukasi” na athari zake kwa shughuli za kawaida.

Msemaji wa polisi, Bw Muchiri Nyaga, alisema vikosi maalum vilitumwa kusindikiza magari katika barabara ya Mwingi–Garissa na kuimarisha usalama kwa wafanyabiashara, wasafiri na wananchi kwa jumla.

Akiwataka wakazi kujizuia, Bw Nyaga aliwahimiza wasiruhusu wahalifu kuvuruga uhusiano mwema ambao umekuwa kati ya jamii hizo kwa muda mrefu.

“Washukiwa hawa hawawakilishi jamii, ukoo wala familia yoyote. Ni maadui wa amani, na vitendo vyao vinakwenda kinyume na maadili ya umoja na ujirani mwema uliowatambulisha Wakenya,” alisema.

Akizungumza Jumatano jioni katika eneo la Ukasi, Mbunge wa Mwingi Kati, Gideon Mulyungi, alisema mvulana huyo wa miaka 14 alikatwa kichwa, tukio lililozua hasira kubwa miongoni mwa wakazi.