Habari za Kitaifa

KMTC yapanua mtaala wake kujumuisha mafunzo ya magonjwa ainati

Na CECIL ODONGO May 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

Chuo cha Mafunzo ya Kimatibabu (KMTC) sasa kimejumuisha vigezo muhimu vya kushughulikia magonjwa mbalimbali yanayochipuka na kushirikisha matumizi ya teknolojia  kwenye mtaala wake wa masomo.

Afisa Mkuu Mtendaji wa KMTC Dkt Kelly Oluoch alisema kuwa mafunzo waliyoyapata kutokana na mkurupuko wa ugonjwa wa corona, umechangia chuo hicho kuanzisha mafunzo ya huduma za dharura, afya ya kiakili na kuhusisha mafunzo ya kiteknojia kwenye mtaala wake.

“Kando na hayo tunalenga kutumia mikakati na mpango wa uuguzi wa kiafya wa jamii, kuwatuma wahudumu wa afya katika maeneo ambayo wapo wachache,” akasema Dkt Kelly Oluoch kwenye kikao na wanahabari. Mafunzo ya teknolojia hasa yanapiga jeki sekta ya utafiti kuhusu maradhi mbalimbali hasa yale yanayoibuka na hatari.

Hivi majuzi KMTC iliruhusiwa kuanza kutoa mafunzo ya kozi za shahada na Mamlaka ya Kitaifa ya Kutathmini Ufaafu wa Vyuo kufundisha kozi maarufu kama KNQA.

Hatua hiyo inawezesha KMTC kuwanoa wauguzi ambao wanaweza kushinda kwenye soko. Chuo hicho sasa kina bewa 92 kote nchini na kinatoa nafasi sawa na mafunzo ya kitaaluma kwa wanafunzi wake wote kote nchini.

Aidha Kmtc inatoa mafunzo kwenye kozi 126 ambazo zinaoana na mahitaji yanayoibuka ya kiafya kama kozi kwenye famasia, afya ya umma, uhandisi kati ya nyanja  nyingine.

“Kwa kipindi kirefu kumekuwa na dhana kuwa Kmtc  inatoa tu mafunzo kwenye kozi za uuguzi na kliniki. Ingawa hizi bado ni msingi imara wa utoaji wa huduma za kiafya, kuna mengi zaidi ambayo taasisi hii inatoa na kuangazia kupiga jeki sekta ya kiafya,” akaongeza.