Jinsi kaunti kame zinavyojenga upya uchumi kupitia kilimo himilivu kwa tabianchi
KWA miaka mingi, ukame, mvua zisizotabirika na upotevu wa mifugo vimekuwa vikitatiza maeneo kame na nusu-kame (ASAL) nchini.
Lakini simulizi hiyo inaanza kubadilika. Badala ya kutegemea mifumo ya jadi ya ufugaji na kilimo ambayo imeendelea kuyumba, jamii za ASAL sasa zinageukia mbinu bunifu na biashara mpya za kilimo himilivu kwa tabianchi—zinazofanikisha sio tu kuishi, bali kustawi.
Katika Kaunti ya Turkana, kwa mfano, Simon Muya alikuwa akitegemea mbuzi na kilimo cha mazao kama ndizi, maboga, pilipili na mboga.
Lakini ukame mkali wa mwaka 2022 ulimuangamizia mbuzi 120, na kumuacha katika hali ngumu ya kujikimu. “Nilipoteza karibu kila kitu,” anakumbuka.
“Lakini kupitia programu ya ustahimilivu dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi, tulianzishiwa kilimo cha moringa. Hapo ndipo safari ya kujijenga upya ilipoanza.”
Muya ni miongoni mwa walionufaika na mradi wa IMARA uliotekelezwa na World Vision Kenya kwa ushirikiano na Ubalozi wa Sweden.
Mradi huo ulifikia karibu watu 73,000 katika kaunti tisa za ASAL, ukilenga kuwasaidia kukabiliana na athari za tabianchi.
Mpango huo wa miaka saba, uliofadhiliwa na Serikali ya Sweden kupitia shirika la Sida kwa gharama ya karibu Sh3.22 bilioni, ulisaidia kufufua zaidi ya hekta 23,000 za ardhi iliyoharibika na kuokoa miti milioni 1.24.
Leo hii, Muya ni mfano wa mabadiliko yanayoshuhudiwa katika maeneo haya. Amegeukia kilimo cha moringa, ufugaji nyuki na uongezaji thamani wa mazao—mbinu zinazostahimili ukame na kumpa kipato bora.

Kwenye mahojiano na Akilimali wakati wa hafla ya kufunga mradi wa IMARA jijini Nairobi, alisema kikundi chao kilianza na robo ekari ya shamba.
Kwa sasa, wanamiliki ekari 17, huku wanachama wakiongezeka kutoka 15 hadi 64. “Sasa tuna miti 500 ya moringa, na karibu kila familia inataka kuipanda,” anasema.
Moringa imejidhihirisha kuwa zao muhimu katika maeneo haya. Hustahimili kiangazi, hutumika kama chakula na pia lishe ya mifugo. “Inapochanganywa na nyasi, huongeza uzalishaji wa maziwa na kuboresha afya ya mifugo,” Muya anaeleza.
Kutokana na mapato ya shughuli hizi, sasa anamiliki mbuzi 270, kondoo 150, ng’ombe 17 na ngamia 22—ishara ya kurejea kwa uthabiti wa kiuchumi.
Aidha, mabadiliko haya yameleta mageuzi katika kijamii. Vijana waliokuwa wakijihusisha na wizi wa mifugo sasa wanajiunga na vikundi vya kuweka na kukopa pesa, kupata mikopo na kuwekeza katika miradi ya kilimo.
“Awali tulikuwa tukiuza unga wa moringa kwa Sh2,000 kwa kilo, lakini sasa bei ni karibu Sh1,600, huku vifurushi vidogo vikiuzwa kwa Sh800,” anaongeza. Kikundi chao huchakata karibu kilo 50 kwa mwezi.
Kilomita nyingi kutoka Turkana, katika Kaunti ya Samburu, hadithi kama hiyo inajitokeza. Silverna Lenturkan, mwenye umri wa miaka 27 na mama wa watoto wanne, alikuwa akitegemea mifugo kabla ya kujiunga na kikundi cha Oporos Beekeepers.
Kupitia mradi wa IMARA mwaka 2018, alipokea mizinga ya kisasa, vifaa vya kuchakata asali na mafunzo ya ufugaji nyuki wa kisasa.
“Nilifunzwa mbinu bora za ufugaji nyuki, na sasa nina mizinga minane inayonipatia kipato cha mara kwa mara,” anasema.
Kikundi chao kilichoanzishwa mwaka 2014 na wanachama 16 sasa kina wanachama 22. Mafunzo hayo, anasema, yamewawezesha wanawake kumiliki na kuendesha shughuli za uzalishaji mali.

Mradi wa IMARA ulitekelezwa katika kaunti za Baringo, Elgeyo Marakwet, Isiolo, Laikipia, Marsabit, Narok, Samburu, Turkana na West Pokot—maeneo ambayo kwa muda mrefu yamekumbwa na changamoto za tabianchi.
Kulingana na Mari Ottosson kutoka Ubalozi wa Sweden jijini Nairobi, juhudi za kukabiliana na athari za tabianchi lazima ziende sambamba na kuimarisha uchumi wa jamii.
“Tumeona vijana wakichukua nafasi ya uongozi katika kuleta mabadiliko kupitia miradi hii,” anasema.
Takwimu za IMARA zinaonyesha ongezeko kubwa la mapato ya jamii—kutoka asilimia 29 hadi 93.1 kufikia Aprili 2026, data hii ikiashiria mafanikio ya mbinu hizi mpya.
Obadiah Kisang wa World Vision Kenya anasema watu 72,994 walinufaika moja kwa moja, karibu nusu yao wakiwa wanawake na wasichana.
“Jamii hizi sasa zinawekeza katika miradi mbalimbali kama vile ufugaji wa nyuki, uzalishaji wa gum Arabic, ufugaji kuku, kilimo cha kahawa, maembe na mazao mengine,” anaeleza.
Aidha, zaidi ya hekta 23,000 zilifufuliwa kupitia upandaji wa nyasi na miti asilia pamoja na kuondoa mimea vamizi.
Vikundi 428 vya akiba vilianzishwa, vikiwa na thamani ya zaidi ya Sh11.39 milioni, hatua inayochochea uwekezaji wa kijamii na kiuchumi.
Miradi ya maji iliyoanzishwa, pia, imepunguza migogoro ya malisho, huku uchimbaji wa visima ukichangia kuimarika kwa amani maeneo yaliyolengwa.