Jinsi Kang’ata alikaa kando ya Rais Ruto Jumapili na kumruka peupe saa chache baadaye
HATUA ya Gavana wa Murang’a, Irungu Kang’ata kutema chama tawala cha UDA huenda ikavutia kisasi kutoka kwa serikali huku Kiongozi wa Wengi Bungeni, Kimani Ichung’wah akitishia kumwaga mtama kuhusu vitendo visivyofaa vya Dkt Kang’ata.
Mbali na kusonga mara kwa mara na kuzama kimawazo alipoketi kushoto mwa Rais William Ruto aliyezuru Shule ya Upili ya Njiiri High, Jumapili, Mei 3, 2026, hakuna kilichoashiria kwamba wawili hao walielekea kufarakana vibaya kisiasa.
Baada ya kuondoka katika hafla hiyo, Dkt Kang’ata aliitisha mkutanao wa vyombo vya habari Nairobi ambapo alitangaza kuwa chama tawala cha Rais hakina ushawishi eneo la Mlima Kenya.
Alitangaza kwamba hatatetea kiti chake katika Uchaguzi Mkuu wa 2027 kwa kutumia UDA iliyomwezesha kushinda 2022.
Baadaye usiku, Dkt Kang’ata alijitokeza kwenye kituo cha televisheni ambapo alifichua kuwa tofauti zake na Rais, UDA na serikali zilianza Julai 2025, na wakati huo vilevile, akamhimiza Bw Ichung’wa akome sarakasi zake na badala yake amtafute wazungumze.
“Nilimtajia rais masuala nyeti niliyofikiri yalikwenda mrama. Nilihoji kwamba anasimamia vibaya siasa za Mlima Kenya kupitia uhasama kisiasa na kukosa kupatia viwanda, elimu na afya kipaumbele inavyotahiki,” alisema, akiongeza kuwa Rais yamkini hakutilia maanani.
Alisema kukua kwa siasa za upinzani Mlima Kenya ni hasara kwa serikali iliyojisababishia yenyewe.
“Kwa Bw Ichung’wah anayedai unafiki kisiasa kunihusu, sitabururwa kwenye mgogoro hadharani. Ni rafiki yangu na anaweza kunitafuta tuzungumze. Baadhi ya masuala anayonuiza yana uzito sana na ninaweza tu kumfafanulia ana kwa ana.”
Dkt Kang’ata amekuwa akishinikizwa vikali na viongozi wa upinzani Mlima Kenya ajitenge na UDA.
Akifahamika kwa sifa yake ya kuwaweka wapigakura kukisia, Dkt Kang’ata amebuni mtindo wa mwanasiasa wa muhula mmoja kwa viti alivyochaguliwa.
Alichaguliwa mara ya kwanza kama diwani 2002 lakini hakutetea kiti chake 2007 alipowania na kushinda kiti cha ubunge cha Kiharu 2013.
Aligombea Useneta Murang’a 2017 na 2022, akawa Gavana wa Murang’a.
Mwaka 2024, alitajwa miongoni mwa watu wenye uwezekano mkubwa kuteuliwa kwa nafasi ya Naibu Rais kufuatia kufurushwa kwa Rigathi Gachagua.
Hata hivyo, Ruto aliishia kumteua Profesa Kithure Kindiki.
“Azma yangu pekee ni kutetea kiti changu 2027, mawazo hayo mengine sina,” alisema.
Katika barua yake mashuhuri ya Disemba 30, 2020, Dkt Kanga’ata alimwonya Rais Kenyatta kuwa mpango wa Kujenga Daraja (BBI) ambao serikali ilifuata kwa kusudi la kura ya maoni haukuwa maarufu Mlima Kenya na ulielekea kusambaratika, akisema hakunuia kuhesabiwa kama mhasiriwa kwenye meli hiyo iliyoelekea kuzama.