Simchukii Oburu, nalinda mwananchi tu, asema Orengo
GAVANA wa Siaya James Orengo amezima uvumi kuhusu mvutano wa kibinafsi kati yake na Oburu Oginga, akisisitiza kuwa kukosoa Chama cha Orange Democratic Movement (ODM) kunatokana na misingi ya kikatiba na si “bifu” la kibinafsi.
Katika mahojiano na runinga moja ya humu nchini Jumatano, Mei 6, 2026, wakili huyo alikosoa uongozi wa sasa wa chama hicho, akidai kuwa ODM imeshindwa kuzingatia kanuni zake za msingi baada ya kifo cha mwanzilishi wake Bw Raila Odinga.
“Sina bifu na Oburu Oginga; si jambo la kibinafsi,” alisema gavana huyo.
“Ninachosema ni kwamba ODM lazima iishi kwa kuzingatia misingi yake na pia lazima iheshimu Katiba.,” aliongeza.
Bw Orengo alidai kuwa kwa mujibu wa kanuni za chama, wadhifa wa juu unapokuwa wazi, mmoja wa manaibu viongozi wa chama anafaa kuteuliwa kuwa kiongozi wa muda hadi uchaguzi mpya ufanyike—mchakato anaodai haukufuatwa baada ya kifo cha Waziri mkuu wa zamani Raila Odinga.
Akisema hakuna kiongozi wa muda rasmi, Orengo alitoa kauli ya kushangaza akisema ametwaa wadhifa huo kuongoza chama kwa dharura.
“Hilo halikufanyika. Lakini kwa kuwa hatuwezi kuwa na pengo la uongozi, mimi ndiye kiongozi wa ODM kwa sasa,” alisema.
Kauli ya kujitangaza kama kiongozi imezidisha mzozo wa ndani ya chama hicho kikubwa cha kisiasa nchini Kenya.
Gavana Orengo ni mmoja wa waanzilishi wa vuguvugu la Linda Mwananchi ambalo limetofautiana na lile na Oburu la Linda Ground.
“Tuna vuguvugu ndani ya ODM linaloitwa Linda Mwananchi,” Orengo alisema, akionesha kuwa vita vya kusaka mwelekeo wa chama bado havijaisha.