Mkutano mkubwa wa Afrika–Ufaransa Nairobi kuwaleta pamoja wajumbe 4,000
MKUTANO mkubwa wa Afrika na Ufaransa unaotarajiwa kufanyika Nairobi utawaleta pamoja zaidi ya wajumbe 4,000 wakiwemo marais 30, wafadhili wa kimataifa, viongozi wa biashara na mashirika ya kiraia.
Huu utakuwa mkutano wa kwanza kama huo kufanyika katika nchi ya Afrika isiyozungumza Kifaransa, hatua inayotajwa kama ya kihistoria katika diplomasia ya kimataifa.
Jana, polisi walitangaza kufungwa kwa barabara kuu na kuimarishwa kwa usalama jijini Nairobi kabla ya Mkutano huo.
Barabara za City Hall Way, Parliament Road, Harambee Avenue na Taifa Road zitafungwa kwa umma kuanzia usiku wa Mei 11.
Aidha, kutakuwa na msongamano wa muda katika Mombasa Road, Thika Road, Limuru Road na Kiambu Road misafara ya wageni ikisafiri kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA) kwenda hoteli na eneo la mkutano.
Kamanda wa Polisi Nairobi, Issa Mohamud, amesema mkutano huo utahudhuriwa na viongozi wakuu wa dunia.
“Tutahakikisha wote wanaohudhuria wanalindwa ipasavyo. Tunawaomba Wakenya waendelee na shughuli zao na kushirikiana na maafisa wa usalama,” alisema.
Alisema Polisi watafanya kazi kwa ushirikiano na Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF), Huduma ya Vijana kwa Taifa (NYS) na vikosi vya usalama vya Ufaransa na Umoja wa Mataifa.
Mkutano huo unatarajiwa kuangazia masuala makuu yanayohusu mustakabali wa Afrika, yakiwemo mageuzi ya madeni na mfumo wa kifedha duniani, mabadiliko ya tabianchi, amani na usalama, pamoja na teknolojia na ubunifu.
Kauli mbiu ya mkutano huo inaendana na ajenda za Rais William Ruto ambazo amekuwa akizisisitiza mara kwa mara katika majukwaa ya kimataifa.
Miongoni mwa wageni wanaotarajiwa ni Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, Mwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika, Mahmoud Ali Youssouf, Mkurugenzi Mkuu wa IMF, Kristalina Georgieva, na Rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, Sidi Ould Tah.
Viongozi wa taasisi za Umoja wa Ulaya pamoja na mashirika mengine ya maendeleo pia wanatarajiwa kuhudhuria.
Serikali ya Kenya inasema mkutano huu ni hatua muhimu ya kidiplomasia ambayo itaweka Kenya katikati ya mazungumzo ya kimataifa kuhusu mustakabali wa Afrika.
Katibu wa Wizara ya Masuala ya Kigeni, Korir Sing’oei alisema mkutano huo unalenga kuanzisha uhusiano mpya kati ya Afrika na Ulaya unaojikita katika ushirikiano unaofaidi pande zote.
“Tunashughulikia mazingira tofauti ya kidunia. Afrika na Ulaya zinapaswa kushirikiana kwa usawa na si kwa misingi ya kihistoria pekee,” alisema Sing’oei.
Mjadala mkubwa utahusu biashara, uwekezaji, utengenezaji wa chanjo, mabadiliko ya tabianchi, usalama wa bahari na maendeleo ya teknolojia.
Aidha, mkutano huo unalenga kuimarisha nafasi ya Afrika kama “bara la suluhisho” badala ya kutegemea misaada.
Ufaransa, ambayo imekuwa ikikosolewa barani Afrika kuhusu mahusiano yake ya kihistoria na mataifa iliyotawala wakati wa ukoloni, inatarajiwa kutumia mkutano huu kuboresha taswira yake.
Rais Emmanuel Macron anasemekana kuwa mstari wa mbele katika kuanzisha mwelekeo mpya wa ushirikiano huo.