WHO yaondoa wasiwasi kuhusu ugonjwa wa hantavirus unaohusishwa na panya
SHIRIKA la Afya Duniani (WHO) jana lilitangaza kuwa mlipuko wa virusi vya hantavirus una hatari ndogo duniani, likisema uwezekano wa maambukizi kusambaa kwa kiwango kikubwa au kusababisha athari kubwa za kiafya bado ni mdogo.
Hadi sasa visa vinane vimeripotiwa, vikiwemo vifo vitatu. WHO imesema visa vitano vimethibitishwa kuwa vya hantavirus huku vingine vitatu vikichunguzwa.
Mkurugenzi wa WHO Kanda ya Afrika, Dkt Mohamed Janabi, alisema mlipuko huo ni ukumbusho kuwa hata magonjwa nadra yanaweza kuyumbisha mifumo ya afya duniani kutokana na kuongezeka kwa safari na utangamano wa binadamu na wanyama.
“Ingawa hatari bado ni ndogo, funzo ni wazi kuwa lazima tuwe tayari,” alisema Dkt Janabi.
Aliwataka viongozi wa Afrika kuimarisha maandalizi na mifumo ya afya, akisisitiza umuhimu wa wahudumu wa afya wenye ujuzi.
Mlipuko huo uliripotiwa kwa mara ya kwanza katika meli ya kitalii ya MV Hondius iliyokuwa ikisafiri kutoka Argentina kuelekea Antarctica na Bahari ya Atlantic Kusini ikiwa na watu 149 kutoka mataifa 23.
Kisa cha kwanza kilishukiwa Aprili 6 baada ya mmoja wa abiria kuugua akiwa safarini. Siku tano baadaye, WHO ilithibitisha kifo cha kwanza.
Virusi vya hantavirus hubebwa hasa na panya na huambukiza binadamu kupitia kinyesi, mkojo au mate ya panya. Maambukizi yanaweza kutokea mtu anapovuta hewa iliyochafuliwa.
WHO imesema aina ya Andes ndiyo iliyobainika katika mlipuko wa sasa, na inaweza pia kusambazwa kutoka mtu mmoja hadi mwingine kupitia mawasiliano ya karibu ya muda mrefu.
Dalili zake ni pamoja na homa, maumivu ya kichwa, misuli kuuma, maumivu ya tumbo, kichefuchefu na kutapika.
Kwa sasa hakuna dawa maalum ya kutibu hantavirus, huku wagonjwa wakitibiwa kulingana na dalili zao.
WHO imeweka watu 69 chini ya uangalizi barani Afrika baada ya kuhusishwa na visa hivyo.
Nchini Kenya, Mkurugenzi Mkuu wa Afya, Patrick Amoth alisema hatari ya ugonjwa huo bado ni ndogo, lakini serikali imeimarisha uchunguzi katika viwanja vya ndege na bandari.
Alisema hakuna kisa kilichoripotiwa nchini hadi sasa na kuwashauri waliotoka mataifa yaliyoathirika kufuatilia afya zao kwa wiki nane.
Katibu wa Afya ya Umma, Mary Muthoni alisema Kenya inaendelea kufuatilia hali hiyo kwa karibu kupitia mifumo ya WHO na kanuni za kimataifa za afya.