Oburu afichua mpango wa kufufua ODM huku akisema yu buheri wa afya
KIONGOZI wa chama cha ODM, Dkt Oburu Oginga, Mei 08, 2026 alijitokeza hadharani baada ya kutoweka kwa takriban wiki mbili na kuwahakikishia Wakenya kuwa yuko salama na mwenye afya njema.
Kutoonekana kwake katika hafla muhimu za chama, ukiwemo mkutano mkubwa wa ODM uliofanyika Mombasa wiki iliyopita, kulizua uvumi kuwa alikuwa akiugua.
Hata hivyo, Dkt Oginga alionekana jijini Kisumu akicheza gofu katika klabu ya Nyanza Golf Club, kuktana na marafiki pamoja na wafuasi wake kabla ya kuzungumza na wanahabari.
Alisema alikuwa Nairobi akishughulikia masuala yake binafsi kabla ya kurejea Kisumu Alhamisi.
“Sikutoweka. Sikukamatwa wala kuteswa. Niko salama, mwenye afya nzuri ” alisema Dkt Oginga.
Aliwashukuru Wakenya kwa kujali hali yake na kusema kuwa aliamua kupumzika kwa muda mfupi huku akiwaachia viongozi wengine wa chama baadhi ya majukumu.
“Huo ndio usimamizi bora. Huwezi kufanya kila kitu ilhali una viongozi uliowapa majukumu,” alisema.
Alisema licha ya kutokuwepo kwake shughuli za ODM zimeendelea vizuri kutokana na chama hicho kuwa na mifumo madhubuti ya uongozi.
Kiongozi huyo pia alifichua mipango ya chama hicho kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Alisema ODM itaanza kufanya mikutano ya hadhara pamoja na mashauriano na makundi mbalimbali ya kijamii, hasa vijana.
“Tutaandaa mikutano ya vijana, wanawake na watu wanaoishi na ulemavu ili kusikiliza maoni yao,” alisema.
Kwa mujibu wa Dkt Oginga, shughuli hizo zitafikia kilele katika mkutano mkuu wa wajumbe wa chama (NDC), ambao utaamua mwelekeo wa ODM kuelekea uchaguzi wa 2027.
“Ikiwa kutakuwa na muungano wa kisiasa, uamuzi huo utafanywa wakati wa NDC. Kama hakutakuwa na makubaliano, chama kinaweza kuamua kwenda uchaguzi kivyake,” alisema.
Aliongeza kuwa kwa sasa ODM inalenga kujipanga na kuimarisha chama badala ya kushughulikia siasa za pembeni.