Habari

Ruto, Gachagua, wang’ang’ania Nyoro 2027 ukikaribia

Na MWANGI MUIRURI May 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MBUNGE wa Kiharu Ndindi Nyoro amejikuta katikati ya mvutano mkali wa kisiasa Mlima Kenya, ambapo mirengo mikuu ya kisiasa inammezea mate kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Baada ya kujijenga kwa takriban miaka 10, Nyoro sasa ameibuka kuwa kigogo katika siasa za eneo hilo.
Rais William Ruto, kiongozi wa Democracy for Citizens Party Rigathi Gachagua, Fred Matiang’i na Babu Owino wote wanamng’ang’ania kisiasa.
Rais Ruto amemwita Nyoro “mwanafunzi wake wa kisiasa”, akionyesha uwezekano wa kushirikiana naye.
Matiang’i naye amedai kushirikiana naye kwa karibu, huku Gachagua akimtaka achague upande wake wazi, akionya kuwa Mlima Kenya haupendi viongozi wasio na msimamo.
Babu Owino amemfungulia mlango wa upinzani. Hata hivyo, Nyoro amechagua kubaki katikati, akisema bado ni mapema kuchukua msimamo kabla ya 2027.
Wachambuzi wa siasa wanasema Nyoro ni mmoja wa viongozi wachache wenye ushawishi mkubwa Mlima Kenya.
Kulingana na mchanganuzi wa siasa Stanley Wang’ombe, yeyote anayempata Nyoro atafaidika kisiasa.
Nyoro, ambaye alichaguliwa mara mbili kwa kura nyingi Kiharu, alipata umaarufu akiwa miongoni mwa vijana waliomuunga mkono Ruto 2018. Hata hivyo, kimya chake katika baadhi ya matukio ya kisiasa kimeongeza presha kwake.