Makala

Udadisi: Mapasta wanavyopigania fungu la kumi, ardhi huku wakiuzia waumini matumaini

Na SIMON CIURI May 12th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

NAKALA za korti na majibizano hadharani imeanika mkondo wa usaliti, vita vya ndani kwa ndani na biashara ya fungu la kumi, huku waumini wakigeuzwa vinyago na wachungaji wanaozidi kujitajirisha na wakiishi maisha ya kifahari kwa kuwauzia matumaini wanajamii wanaoshawishika kwa urahisi.

Udadisi wa Taifa Leo umefichua vita vikali ndani ya kanisa huku mapasta wakizozania fungu la kumi, matawi na ardhi.

Mapasta James Ng’ang’a almaarufu Kamanda wa Kanisa la Neno Evangelism, Ben Kiengei wa Jesus Compassionate Ministry (JCM) International, Pius Muiru wa Maximum Miracle Centre na James Wanjohi wa Jesus Culture Ministry ni miongoni mwa walioangaziwa.

Nakala za korti zilizofikia Taifa Leo zinafichua kuwa Pasta Ng’ang’a ana kesi kortini kupigania udhibiti wa kanisa na mali yenye thamani ya Sh6 milioni Kitengela, baada ya kudaiwa kuingia kwenye mkataba ambao ungewezesha kufungua tawi kaunti ya Kajiado.

Baada ya mkataba huo, Pasta Samuel Munene Muriithi alifungua kanisa la kujitenga na kuliita God’s Love Assembly Church.

Katika uamuzi wake, Jaji Christine Ochieng anasema Neno Evangelism haikuthibitisha kuwa Pasta Muriithi alihamisha ardhi inayozozaniwa kwa mhusika wa tatu, akitaja suala hilo kuwa mgogoro kuhusu usimamizi wa kanisa wala si mzozo wa ardhi.

Kaunti ya Kiambu, Ruiru, mchekeshaji wa zamani aliyegeuka kuwa pasta, Askofu Ben Kiengei amejipata katika hali sawia ambapo pesa na fungu la kumi limesababisha baadhi ya mapasta wake kutema JCM na kuanzisha makanisa yao binafsi.

Aprili 22, mwaka huu Rais William Ruto alizuru JCM na kuahidi ShSh8 milioni zilizochochea mgogoro unaoendelea kati ya Askofu Kiengei na Pasta Charles Wachira, aliyeongoza JCM International.

Bw Wachira alijiuzulu ghafla baadaye akitaja ukosefu wa maadili katika kanisa hilo.

Pasta Muiru vilevile amepigwa na bumbuwazi baada ya kutapeliwa katika biashara ya fungu la kumi huku akipigania kuokoa mali yake yenye thamani ya Sh960 milioni isipigwe mnada kufuatia mgogoro kuhusu mkopo wa Sh216 milioni na Benki ya Equity kuanzia 2020 wakati wa janga la 2020.

Pasta Muiru amesalitiwa katika mkataba mwingine na kupoteza kesi ambapo alimshtaki pasta mwenza wa Maximum Miracle Centre. Uhasama huo ulianza miaka michache baada ya kumtawaza Andrew Mlewa Mkare.

Eneo la Marurui, Roysambu, Nairobi, Pasta Wanjohi amefunga kanisa lake la Jesus Culture Ministry.

Wanjohi si mgeni kwenye utata. Aprili 22, 2024, aliangaziwa na Taifa Leo baada ya kampuni zake mbili WorthStart Africa na Worthstart Travel Agency kuwatapeli wasaka kazi, wakiwemo wafuasi wa kanisa lake Sh600 milioni baada ya kuahidiwa kazi ng’ambo.

Nchini Kenya, sheria za kudhibiti makanisa ni maandishi pekee na kadri kanisa linavyoweza kuvutia umati, ndivyo linavyovutia wanasiasa zaidi wanaofurika wakiahidi sadaka ili kupata wafuasi kisiasa ambapo sadaka huishia mikononi mwa watu wachache.