Dhiki ya mafuriko yatua tena Tana River maji yakitishia kusomba vijiji na mifugo ‘wakati wowote’
GAVANA wa Tana River, Bw Dhadho Godhana na Kamishna wa Kaunti hiyo Joseph Mwangi wametoa tahadhari mpya kwa wakazi wanaoishi maeneo yanayokumbwa na mafuriko kuhama na kuelekea maeneo ya juu ili kuepuka kuathiriwa na mafuriko makubwa yanayotabiriwa katika siku na wiki zijazo.
Haya yanajiri huku kina cha maji ya Mto Tana unaopita maeneo mengi ya Kaunti ya Tana River kikizidi kuongezeka.
Gavana Godhana alisema serikali ya kaunti imetambua maeneo salama na kuanzisha kambi za dharura zenye makazi ya muda kwa ajili ya maandalizi ya mafuriko hayo.
Kulingana naye, kampuni ya kuzalisha umeme ya KenGen huenda ikaanza kuachilia maji ya ziada kutoka kwenye mabwawa yake wakati wowote kutokana na mvua kubwa zinazoendelea kunyesha maeneo ya juu, hali inayoongeza hatari ya mafuriko zaidi.
“Ninawasihi wale wanaoishi karibu na kingo za mto na maeneo ya chini kuhama kwa sababu kiwango cha maji kitaongezeka ghafla na kuhatarisha maisha,” alisema.
Mkuu huyo wa kaunti aliahidi kuwapa waliohamishwa chakula, blanketi, matandiko na huduma za dharura za matibabu.
Bw Godhana alisema hatua hizo za muda zimechukuliwa huku mipango ikiendelea ya kuwahamishia baadaye katika vijiji vilivyotambuliwa.
Pia alitangaza kuwa ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, zinazolenga kusaidia jamii ambazo huathiriwa mara kwa mara na mafuriko, utaanza mwezi huu.
Kwa upande wake, Bw Mwangi, aliwataka wakazi kufuata kikamilifu maagizo ya kuhama kutokana na hatari ya mafuriko makubwa.
Alisema machifu na wasaidizi wao wanaendelea kuwafahamisha wakazi kujiandaa kwa mafuriko yaliyotabiriwa, akibainisha kuwa viongozi hao wa mashinani watasaidia kuwaondoa watu walio katika hatari.
“Mafuriko kwa kawaida huacha uharibifu mkubwa na kuvuruga maisha ya wananchi, na tunawaomba wale wanaoishi maeneo ya mafuriko kuhamia maeneo ya juu kutokana na kuongezeka kwa kina cha maji,” alisema.
Bw Mwangi pia aliwashauri wafugaji wanaoishi karibu na kingo za mto kuwahamisha mifugo wao hadi maeneo salama.
Vikosi vya shirika la Kenya Red Cross vimeanzisha operesheni ya uokoaji na utathmini, vikivuka eneo la Laga Galole lililofurika katika kivuko cha Daba ili kufika kijiji cha Gofisa katika Kaunti Ndogo ya Galedertu hivi majuzi, ambako familia kadhaa zilikuwa zimekwama kutokana na kuongezeka kwa maji ya mafuriko.
Katika taarifa, shirika hilo lilisema tathmini zilizofanywa zimebaini kuwa angalau familia 81 zimeathirika, huku mahitaji ya dharura yakijumuisha chakula, huduma za matibabu na vyandarua kutokana na kuongezeka kwa hatari ya magonjwa.
Bw Mwangi alisema tathmini hizo zimethibitisha kuwa familia 81 zimeathirika katika Kaunti Ndogo ya Galadertu na zinahitaji msaada wa chakula, huduma za matibabu na vyandarua kutokana na kuongezeka kwa hatari za kiafya.
Hatua hiyo inajiri wakati serikali ikitoa tahadhari mpya za mafuriko kwa wakazi wa kaunti za Garissa na Tana River kuhusu kuongezeka kwa kina cha maji ya mito na uwezekano wa kufurika kutokana na mvua inayoendelea kunyesha maeneo ya juu ya mito hiyo.