NI RASMI: Dollarline wa UDA ashinda kiti cha ubunge cha Emurua Dikirr akimbwaga Vincent wa DCP
MWANIAJI wa UDA David Kipsang Keter ametangazwa mshindi wa uchaguzi wa eneobunge la Emurua Dikirr baada ya Tume ya Uchaguzi na Mipaka IEBC kukamilisha zoezi la kuthibitisha na kuhesabu kura.
Kulingana na IEBC, Bw Keter anayefahamika na wafuasi wake kama Dollarline amejizolea kura 18,266 dhidi ya mpinzani wake mkuu mkuu, Vincent Rotich almaarufu ‘Pinceent’ wa DCP aliyejipatia kura 10,760.
Wengine walioshiriki uchaguzi huo ni Gideon Koech wa chama cha NVP aliyejipatia kura 190, Cherono Desma wa PNU aliyepata kura 80 na Kiprono Rotich wa chama cha RLP aliyeridhika na kura 62.
Uchaguzi huo ambao ulikuwa umepigiwa upatu kuwa wa vita vya ubabe kati ya Rais William Ruto na aliyekuwa Naibu wake aliyegeuka hasimu mkuu Rigathi Gachagua ulikumbwa na ghasia awali, ingawa polisi waliingilia kati na kutuliza hali.
Katika kipindi fulani wakati shughuli ya kuhesabu kura ilipoanza, polisi walilazimika kurusha vitoa machozi kutawanya wafuasi, wengi wao wa UDA waliokuwa wameanza kuzingira kituo cha kuhesabu kura.
Uchaguzi huo mdogo uligeuka kuwa kipimo muhimu cha nguvu za kisiasa kati ya chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA) na chama kipya cha Democracy for Citizens Party (DCP) kinachoongozwa na Bw Gachagua.
Rais Ruto alitaka chama chake kihifadhi kiti hicho kilichobaki wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge Johana Ng’eno, huku Bw Gachagua alitarajia kupata ushindi wa kwanza wa chama chake katika Bunge la Kitaifa.
Bw Ng’eno alifariki Februari 28, 2026 baada ya helikopta aliyokuwa akisafiria kuanguka katika eneo la Mosop, Kaunti ya Nandi.
Katika ajali hiyo, rubani George Were, mpiga picha Nick Kosgei, mwalimu Carlos Kibet Keter, askari wa Huduma ya Misitu Kenya (KFS) Amos Kipngetich Rotich na afisa wa itifaki wa serikali ya Narok Wycliff Kiprotich Rono pia walipoteza maisha.