Habari

Dollarline wa UDA achukua usukani kura zikiendelea kuthibitishwa na kuhesabiwa Emurua Dikirr

Na VITALIS KIMUTAI May 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MWANIAJI wa kiti cha ubunge cha Emurua Dikirr kwa tikiti ya UDA David Kipsang Koech amechukua uongozi wa mapema kura zikiendelea kuthibitishwa na kuhesabiwa na IEBC.

Kufikia 1.11am, David Koech anayefahamika maarufu kama Dollarline alikuwa anaongoza kwa kura 11,643 huku mpinzani wake mkuu, Vincent Rotich almaarufu ‘Pinceent’ wa DCP alikuwa na kura 7,839.

Kura hizi zilitokana na vituo 64 kati ya 94 vilivyokuwa vimehesabu kura kufikia muda huo.

Awali, watu wanne walijeruhiwa baada ya wafuasi wa Chama cha United Democratic Alliance (UDA) na Democracy for Citizens Party (DCP) kuvurugana katika uchaguzi huo mdogo wa Emurua Dikirr uliofanyika Alhamisi.

Kwa mujibu wa polisi, tukio hilo lilitokea karibu na vituo vya kupigia kura vya Chelemei na Kiribwet katika wadi ya Kapsasian, ambapo waliojeruhiwa walikimbizwa katika hospitali mbalimbali kupatiwa matibabu.

Tukio hilo lilitokea wakati wapiga kura 44,457 wa eneo bunge la Emurua Dikirr, Kaunti ya Narok, walipokuwa wakiendelea kupiga kura kumchagua mrithi wa aliyekuwa Mbunge wa awamu tatu Johana Ngeno.

Tume ya IEBC iliwaidhinisha wagombeaji David Kipsang Keter (UDA), Desma Cherono (PNU), Vincent Rotich (DCP), Gideon Koech (NVP) na Kenneth Kiprono (RLP).

Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Narok Patrick Lobolia alithibitisha vurugu kati ya wafuasi wa UDA na DCP, huku wagombea wakitoa wito wa utulivu na kuimarishwa kwa usalama kuzuia kuongezeka kwa mvutano.