Tahadhari Uganda ikithibitisha kisa cha kwanza cha Ebola, vifo 80 vikiripotiwa DRC
UGANDA imethibitisha kisa kimoja cha maambukizi ya Ebola, wakati watu 80 tayari wameripotiwa kufariki katika mlipuko unaoendelea katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), mamlaka za afya zimeeleza.
Wizara ya Afya ya Uganda ilisema kisa hicho kilihusisha mwanaume mmoja mwenye asili ya Congo ambaye aliingia nchini humo na baadaye kulazwa hospitalini mjini Kampala, ambapo alifariki dunia baada ya kuthibitishwa kuwa na Ebola aina ya Bundibugyo.
Maafisa wamesema hatua za ufuatiliaji wa watu aliokutana nao zimeanza ili kuzuia uwezekano wa maambukizi zaidi.
Wakati huo huo, Shirika la Afya la Afrika (Africa CDC) limesema mlipuko wa Ebola katika jimbo la Ituri, mashariki mwa DRC, umeendelea kusababisha vifo 80.
Mlipuko huo umeathiri zaidi maeneo ya Mongwalu na Rwampara, ambayo ni miji inayojulikana kwa shughuli nyingi za uchimbaji wa dhahabu.
Maafisa wa afya wanasema mazingira hayo ya msongamano wa watu na kutagusana mara kwa mara kati ya jamii mbalimbali yanaongeza hatari ya kuenea kwa haraka kwa virusi hivyo, ambavyo tayari vimekuwa vikiripotiwa katika milipuko kadhaa nchini DRC kwa miaka mingi.
Uganda imeimarisha usalama wake katika mipaka yake na DRC, huku timu za dharura za afya zikiwekwa tayari kugundua na kudhibiti visa vipya vinavyoweza kuingia nchini humo.
Hatua hizo zimechukuliwa kutokana na historia ya maambukizi ya kuvuka mipaka katika eneo hilo la Afrika Mashariki, ambapo watu husafiri mara kwa mara kwa biashara na shughuli za kijamii.
Kwa mujibu wa wataalamu wa afya, Ebola ni ugonjwa hatari unaosambazwa kupitia ukaribu wa moja kwa moja na majimaji ya mwili wa mtu aliyeambukizwa au vitu vilivyochafuliwa.
Ugonjwa huo huanza kwa dalili kama homa kali, maumivu ya misuli, uchovu na maumivu ya kichwa, kabla ya kuendelea na kutapika, kuharisha, vipele na wakati mwingine kutokwa na damu.
Shirika la Afya Duniani (WHO) linasema Ebola ina kiwango cha vifo kinachokadiriwa kufikia asilimia 50, ingawa kiwango hicho kinaweza kutofautiana kulingana na upatikanaji wa huduma za matibabu na kasi ya kugundua maambukizi.
Africa CDC imesema inaandaa mikutano ya dharura na serikali za DRC, Uganda na Sudan Kusini pamoja na washirika wa kimataifa ili kuimarisha doria mipakani, usambazaji wa vifaa vya afya na elimu kwa jamii ili kupunguza maambukizi zaidi.
Wakati mamlaka zikijaribu kudhibiti hali hiyo, hofu imeendelea kuongezeka kutokana na mwendo wa kasi wa maambukizi katika maeneo ya mijini na ya mipakani, ambako watu wengi hutangamana kila siku bila kinga ya kutosha dhidi ya virusi hivyo hatari.