Habari

SIASA: Mvutano viongozi wakionya ODM kuhusu tikiti ya ugavana Kisumu

Na CECIL ODONGO May 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BAADHI ya viongozi wa ODM kutoka Kaunti ya Kisumu wameonya chama hicho kwamba hawatakubali demokrasia ya maafikiano katika kinyang’anyiro cha ugavana mnamo 2027, wakisisitiza kuwa wapigakura lazima wapewe nafasi ya kuchagua viongozi wanaowataka.

Wakiongozwa na Mbunge wa Muhoroni, James Onyango K’Oyoo, Mbunge wa Kisumu Kati, Joshua Oron, pamoja na zaidi ya wanachama 20 wa Bunge la Kaunti ya Kisumu (MCAs), viongozi hao wameapa kupinga msimamo wa chama na kufuata mkondo wao wa kisiasa iwapo uteuzi wa mgombea wa ugavana hautakuwa wa haki na huru.

Bw K’Oyoo, ambaye anaunga mkono azma ya Dkt Oron ya kuwania ugavana, alianza kwa kutangaza kuwa hawatakubali uamuzi wowote wa vikao vya siri ambao utampa mgombea mwengine tiketi ya moja kwa moja.

“Tunataka kuambia ODM kwamba wakati huu hakuna mambo ya mtu kuletwa na cheti. Cheti pekee tutakachokubali ni chako wewe (Dkt Oron) kwa sababu ya yale ambayo umefanya na uungwaji mkono ulio nao kwa sasa,” akasema Bw K’Oyoo.

Alikuwa akizungumza katika uwanja wa Shule ya Upili ya Withur, wadi ya Kabonyo Kanyagwal eneobunge la Nyando.

Hafla hiyo ilitumiwa na ukoo wa Kano kutoka Kaunti ndogo ya Kadibo kutangaza kuwa wanaunga mkono azma ya Dkt Oron wakimtaja kama kiongozi ambaye atatimiza miradi ya maendeleo na kuinua eneo hilo kisiasa.

“Kama ilivyo Nyando, Muhoroni pia inaunga mkono Dkt Oron na tunajua kuna watu watakuja na pesa, lakini waelewe kuwa wakati huu hatutabadili msimamo wetu kwa sababu ya shinikizo kutoka kwa chama,” akaongeza Bw K’Oyoo.

Kinyang’anyiro cha ugavana wa Kisumu kimezua ushindani mkali ndani ya ODM, huku suala la usawa wa uwakilishi wa maeneo likitawala mijadala ya kisiasa miongoni mwa wanaotafuta kuungwa mkono.

Mbali na Dkt Oron, wengine waliotangaza nia ya kuwania kiti hicho ni Seneta wa Kisumu Tom Ojienda, Naibu Gavana wa Kisumu, Mathews Owili, Mbunge wa Nyakach Aduma Owuor, Gavana wa kwanza wa Kisumu Jack Ranguma, pamoja na aliyekuwa Mbunge wa Kisumu Kati Ken Obura.

Gavana Anyang’ Nyong’o, ambaye anahudumu muhula wake wa pili na wa mwisho, amekuwa kimya na hajatangaza hadharani mwaniaji anayemuunga.

“Nina matumaini kwamba nitawashinda wapinzani wangu ndani ya ODM kwa sababu hata kabla ya kuchaguliwa kuwa mbunge, nilikuwa nikifanya kazi kwa ajili ya watu wetu. Miradi niliyoanzisha na kukamilisha hapa Nyando ipo wazi kwa kila mtu kuona, na nitakapokuwa gavana, kazi yangu ya kwanza itakuwa kuboresha miundombinu ambayo ni duni katika eneo hili,” akasema.

Bw Oron ambaye anahudumu muhula wake wa kwanza.

Mwanasiasa mkongwe wa Nyando Lumumba Ouya ‘Kalausi’ alisema kuna wagombea wengine wa ugavana wanaowachanganya wapigakura na wanapaswa kupuuzwa.

Hafla hiyo ilihudhuriwa na zaidi ya madiwani 20 wa Bunge la Kaunti, aliyekuwa mgombea wa ugavana na sasa anayewania ubunge wa Muhoroni Dkt Hezron Mc’Obewa, ambaye alivutia hisia mnamo 2017. baada ya kuongoza kampeni ya ugavana iliyokuwa ya kifahari na iliyopangwa kwa ustadi mkubwa.