Mafuriko: Familia zalalamikia hama-hama wakati wa mvua
FAMILIA zinazoishi katika maeneo ambayo huathiriwa na mafuriko Kaunti ya Tana River, zimetaka serikali itafute suluhisho la kudumu ili kushughulikia suala la kuhama kila mara mvua nyingi inaponyesha maeneo ya juu nchini.
Katika kijiji cha Bularahma kilicho Galili, Tana Delta, maji ya mafuriko yamezamisha mashamba na kuacha makazi yakiwa yamezingirwa na maji kiwango cha maji kwenye Mto Tana kikipanda.
Mafuriko hayo pia yanahusishwa na maji kufurika kutoka baadhi ya mabwawa ya Seven Forks yanayotumiwa kuzalisha umeme na kampuni ya KenGen.
“Maji yalijaa yakaharibu mashamba yetu. Tulikuwa tumepanda mboga, nyanya na matunda lakini kila kitu kikaharibika,” Bi Nina Ali Kulo, mkazi, alisema akikadiria hasara.
Familia zinazoishi katika kijiji hicho zinajiandaa kuhama, na kutatiza tena maisha yao.
Bw Said Zajardul anasema jamii zilihamia kijiji hicho baada ya kuhamishwa na mafuriko eneo la Gamba.
Makumi ya makazi yameathirika katika eneo hili pekee.
“Sasa wanalazimika kuhama tena. Wamekata miti ili waende kujenga kwingine. Wameteseka kwa zaidi ya miaka 12,” akasema Bw Zajardul.
Katika kijiji jirani cha Lango la Simba, Bw Joseph Masila anatumia mashua yake ndogo kupitia maji ya mafuriko akitafuta vifaa vya ujenzi.
Anasema kuhama mara kwa mara ni mzigo mkubwa wa kiuchumi na unaumiza sana familia ambazo tayari zinapitia ugumu.
“Kila mara unapohama unalazimika kuanza upya. Wakati utakaporejea kwako pia utakuta mali ulizoacha zimeharibika, kwa hivyo utaanza tena maisha,” akasema kwa masikitiko.
Kwa mujibu wa wakazi, mafuriko yanaleta pia mamba na nyoka, pamoja na magonjwa ya maji na yale yanayoenezwa na mbu.
Bw Masila anasema usumbufu huu wa mara kwa mara pia umeathiri elimu katika eneo hilo.
Bw Mohamed Golo ni miongoni mwa mamia waliotoka kijiji cha Bandi huko Gamba, lakini akalazimika kuhama tena baada ya mafuriko kuharibu makazi yao ya muda upande mmoja wa barabara Minjila.
Karibu watu 400 wamehamia eneo la Minjila kwa usalama wao, na sasa wanalazimika kuishi upande mmoja wa barabara ambao hauathiriwi na mafuriko.
Bw Golo anasema serikali ya kaunti iliruhusu wajenge nyumba hapo, lakini wengi ni maskini na hutegemea mahema yaliyotolewa na Shirika la Kenya Red Cross.
Bw Bobode Ali, mmoja wa waliokumbwa na mafuriko, alieleza changamoto za kutegemea mahema kama makazi.
“Hizi hema tulipewa na Red Cross lakini sasa zimetoboka. Mvua inaponyesha, huwa kwavuja ndani. Pia kuna joto jingi humo ndani, kisha wazazi na watoto wote wanalala kwa hema moja, hakuna usiri,” akaeleza.
Katika kambi hizo, wanategemea sana wahisani kwa chakula, maji safi na mahitaji mengine muhimu kama vile vyandarua na dawa.
Hali hii kwa familia ambazo zimezoea kujitegemea inawapokonya utu wao.
Wakazi wengi wamebaki wakijiuliza kwa nini mabwawa hayawezi kujengwa kuhifadhi maji badala ya kuyaacha yaelekee Bahari ya Hindi.
Serikali ya Kaunti ya Tana River ilishauri waathiriwa kuhamia maeneo ya juu huku juhudi zikifanywa kuweka suluhu za kudumu.
Gavana Dhadho Godhana alisisitiza kuwa, serikali ya kaunti ina mpango unaoendelea wa kuwahamisha wakazi wanaoishi katika maeneo hatari kwenda katika vijiji salama watakavyojengewa.