Waziri wa Fedha, John Mbadi. Picha|Maktaba
WAZIRI wa Fedha John Mbadi, amemulikwa baada ya wabunge kumuagiza kufika mbele yao kufafanua uhamisho wenye utata wa taasisi za kitaifa zilizo chini ya Wizara ya Kawi kwa Hazina mpya ya Miundomsingi ya Kitaifa.
Wanachama wa Kamati ya Nishati, vilevile, walisimamisha kikao cha kusikiza makadirio ya bajeti kwa Wizara ya Kawi na Petroli, ambayo walisema imepunguzwa pakubwa kufuatia uhamisho huo.
Kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Nakuru Mashariki, David Gikaria, ilisema uhamisho wa Kampuni za Kuzalisha Umeme Nchini (KenGen), Kenya Power (KP), Ketraco, na Geothermal Development Company (GDC) kwa NIF pasipo idhini zinazofaa ni kukiuka wajibu wake.
Hatua ya ghafla ya kuorodhesha upya taasisi za kitaifa imezua pingamizi kali kutoka kwa Katibu wa Wizara ya Nishati Alex Wachira na Katibu wa Wizara ya Petroli, Mohamed Birick, waliofika mbele ya kamati kuwasilisha makadirio ya bajeti yao mwaka ujao. Makatibu hao wawili walilalamikia uhamisho wa asasi hizo zilizosababishwa kusitishwa kwa mikutano iliyopangwa kujadili mabadiliko ya bajeti.
Wanakamati walionya kuwa kuhamisha GOE katika idara tofauti kunapunguza pakubwa bajeti ya Wizara ya Nishati, na kuhatarisha miradi kadhaa ya mabilioni inayofadhiliwa na wahisani. “Halitakuwa jambo la busara kwetu kuketi hapa na kuidhinisha bajeti kwa matumizi ya sasa pekee. Haifai. Tunataka Waziri wa Hazina Kuu na Katibu wa Wizara waje hapa na kufafanua suala hili,” alisema Bw Gikaria.
Kulingana na Bw Gikaria, uhamisho ‘haramu’ wa GOEs na bajeti zao kwa NIF, ambayo bado haijaanza kutekelezwa, unazua tishio la kusababisha waajiriwa wa wizara kupunguzwa na umekosolewa na Afisi ya Bajeti ya Bunge (PBO) kama inayotatiza mchakato wa kuunda bajeti kikatiba.
Katika Nakala ya Sera ya Bajeti (BPS) 2026 iliyoidhinishwa na Bunge la Kitaifa Machi 2026, Idara ya Kawi ilikuwa na kipimo cha matumizi cha Sh78.3 bilioni kwa mwaka wa kifedha2026/27, ikiwemo Sh13.3 bilioni za matumizi ya kila siku na Sh64 bilioni kwa maendeleo.
Hata hivyo, kufuatia uhamisho wa GOE kwa NIF, makadirio ya bajeti ya Wizara yaliyowasilishwa bungeni yamepunguzwa hadi Sh31.52 bilioni zinazojumuisha Sh13.3 bilioni za matumizi ya kila siku na Sh18.2 bilioni za maendeleo. “Tupo hatarini. Hata kama tunataka kuhamia NIF, inapaswa kuwa kwa hatua. Tunaomba bajeti irejeshwe,” alisema Katibu wa Wizara Wachira.