Maswali tele kuhusu wamiliki wa magari ya Prado yanayotumiwa na wahuni
WALITUMIA kasi, vurugu na barakoa kutekeleza operesheni yao walipovamia mji wa Ol Kalou wakati wa uchaguzi mdogo wa ubunge uliofanyika Alhamisi.
Baada ya kuchanganua video zilizothibitishwa, msururu wa matukio na taarifa kutoka vyanzo vya wazi, Taifa Jumapili ilifuatilia baadhi ya mambo ambayo wanaume hao waliovaa barakoa na kufunika nyuso walitaka kuficha walipokuwa wakirushia wakazi vitoa machozi na kuwashambulia wanahabari.
Uchunguzi ulibaini kuwa gari aina ya Toyota Land Cruiser jeusi lilikuwa likiongoza msafara wa magari mengine yaliyokuwa yakiwabeba baadhi ya wanaume hao. Gari hilo lilikuwa na nambari ya usajili KDL 477Q.
Rekodi zinaonyesha kuwa nambari hiyo imesajiliwa kwa jina la John Njuguna Wanjiku, jina linalofanana na la Mbunge wa Kiambaa.
Video iliyorekodiwa na mkazi mmoja inaonyesha mwanaume anayefanana na Bw Wanjiku akiwa kando ya Land Cruiser hiyo.
Anaonekana akizungumza na kundi la wanaume kabla ya mmoja wao aliyefunika uso kwa barakoa, skafu na kofia ya mavazi ya kijeshi kumfungulia mlango wa gari.
Katika mahojiano na Taifa Jumapili, Bw Wanjiku alikiri kuwa ndiye aliyeonekana kwenye video na kwamba gari hilo ni lake. Hata hivyo, alikanusha kuhusika na makosa yoyote.
Alisema alikuwa akizunguka Ol Kalou akimuunga mkono mgombeaji wa UDA alipokumbana na wahuni.
“Nilikuwa na mlinzi wangu binafsi, msaidizi na wapiga picha wangu. Tulikwama barabarani kwa sababu ilikuwa imefungwa kwa mawe. Tuliposhuka kuyaondoa, kulikuwa na wahuni upande mwingine na maisha yetu yalikuwa hatarini. Tulilazimika kurudi nyuma. Tulipofika karibu na kituo cha kupigia kura cha AC tulikuta magari ya Prado yaliyokuwa na watu waliodaiwa kuwa magenge. Sisi tulikuwa tunajaribu kutoroka baada ya kupiga doria eneo hilo,” alisema.
Aliongeza kuwa alikuwa Ol Kalou kwa zaidi ya mwezi mmoja akihakikisha maajenti UDA wako salama.
Kwenye video hiyo, Land Cruiser ya Bw Wanjiku inaandamana na Toyota Harrier nyeupe yenye nambari KDX 410K.
Uchunguzi wa Taifa Jumapili ulionyesha kuwa gari hilo limesajiliwa kwa kampuni ya MKS Investments, inayojihusisha na uagizaji na uuzaji wa magari. Rekodi zaidi zinaonyesha kampuni hiyo inamilikiwa na Khalique Mansoor, raia wa Pakistan.
Bw Wanjiku alisema kwa mtazamo wake, waliokuwa ndani ya gari hilo huenda walitoka kambi nyingine ya kisiasa na walikuwa wakitoroka wahuni.
Taifa Jumapili iliwasiliana na MKS Investments kuuliza iwapo gari hilo lilikuwa lao na kwa nini lilionekana katika tukio hilo, lakini haikupata majibu kufikia wakati wa kuchapishwa kwa taarifa hii.
Katika eneo jingine karibu na kituo cha kupigia kura, Land Cruiser nyingine nyeusi yenye nambari KDW 600Q ilionekana ikiwabeba wanaume waliovalia barakoa.
Uchunguzi ulibaini kuwa nambari hiyo imesajiliwa kwa Vipingo Industries Limited, kampuni yenye makao Mtwapa, Kaunti ya Kilifi, inayotengeneza bidhaa kama unga wa Dola, mafuta ya kupikia ya Golden Drop na sabuni ya Vipingo Cream.
Hata hivyo, kwenye mfumo wa Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi na Usalama Barabarani (NTSA), nambari hiyo imeorodheshwa kuwa ya Toyota Station Wagon nyeupe, huku aina kamili ya gari ikiwa haijawekwa.
Taifa Jumapili iliwasiliana na Vipingo Industries kuuliza iwapo gari hilo lilikuwa lao na kwa nini lilihusishwa na tukio hilo.
Kampuni hiyo ilijibu kuwa haina Land Cruiser nyeusi yenye nambari hiyo wala gari lingine lolote la aina hiyo.
Badala yake, ilisema inamiliki Toyota Probox nyeupe yenye nambari hiyohiyo ya usajili KDW 600Q.
Hii iliibua maswali kuhusu jinsi nambari moja ya usajili inaweza kuonekana kwenye magari mawili tofauti.
NTSA ilipohojiwa ilisema hutenga nambari moja kwa gari moja pekee.
Mamlaka hiyo iliongeza kuwa matumizi ya nambari bandia au za kughushi ni uhalifu unaohatarisha usalama wa umma.