Wantam: Sifuna sasa alenga kupambana na Ruto 2027 baada ya kuvuliwa wadhifa
KAULI ya Seneta wa Nairobi, Edwin Sifuna, kwamba yuko tayari kuwania urais mwaka 2027 limepatia sura mpya siasa za upinzani na kuzua mjadala kuhusu mustakabali wa vuguvugu la Linda Mwananchi.
Akizungumza katika mkutano wa kisiasa uliofanyika Mwatate, Kaunti ya Taita Taveta, Jumamosi, Sifuna alisema licha ya kupokonywa nyadhifa zote alizopewa ndani ya ODM, vijana wa Kenya wako tayari kumpa nafasi kubwa zaidi ya kuongoza nchi.
“Wameninyang’anya kila kitu Baba alinipa. Wameniondoa kama Naibu Kiranja wa Wachache katika Seneti na pia wameniondoa kwenye wadhifa wa Katibu Mkuu wa ODM. Lakini vijana wamesema watanipa cheo cha kuitwa mtukufu,” alisema, akimaanisha urais.
Kauli hiyo imejiri siku chache baada ya Spika wa Seneti, Amason Kingi kutangaza mabadiliko ya uongozi wa wachache, yaliyomwondoa Sifuna kama Naibu Kiranja wa Wachache na nafasi yake kuchukuliwa na Seneta wa Migori Eddy Oketch.
Sifuna alisema nyadhifa zinaweza kuondolewa lakini haziwezi kufuta uungwaji mkono anaopata kutoka kwa Wakenya.
“Vyeo wanaweza kuninyang’anya, lakini hawawezi kuninyang’anya akili yangu wala uungwaji mkono wa wananchi. Uongozi unatokana na wananchi,” alisema.
Aidha, alisema Linda Mwananchi inalenga kurithi kura pamoja na viti vya ODM katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Kauli hiyo imezua hisia kwamba vuguvugu hilo linaanza kujigeuza kutoka kundi la kushinikiza mabadiliko hadi jukwaa la kisiasa linaloweza kusimamisha mgombea wa urais.
Hata hivyo, wachambuzi wa siasa wanasema Linda Mwananchi bado inakabiliwa na changamoto nyingi kabla ya kuwa nguvu ya kitaifa.
Changamoto kubwa ni kwamba haijasajiliwa kama chama cha kisiasa, hivyo haiwezi kusimamisha wagombeaji katika uchaguzi.
Msajili wa Vyama vya Kisiasa aliwahi kukataa ombi la kukisajili.
Wanaweza kuendelea kushinikiza kisajiliwe, kujiunga na chama kilichosajiliwa au kurejea ODM na kujaribu kukidhibiti kutoka ndani.
Vuguvugu hilo pia linawakutanisha viongozi kutoka vyama tofauti kama ODM, Wiper, Jubilee pamoja na wanasiasa huru ambao wameunganishwa zaidi na upinzani wao dhidi ya serikali ya Rais William Ruto.
Tofauti hiyo ya kisiasa imeonekana kuwa nguvu yake, lakini pia inaweza kuwa chanzo cha migogoro kuhusu uongozi na mgombeaji wa urais.
Gavana wa Siaya James Orengo, ambaye ni mmoja wa vinara wa Linda Mwananchi, pia amedokeza kuwa vuguvugu hilo lina mgombea wake wa urais.
“Nani amesema Linda Mwananchi haina mgombeaji wa urais?” aliwauliza wafuasi katika mkutano huo.
Kauli hiyo imezua maswali iwapo Orengo naye ana azma ya kuwania urais au atamuunga mkono Sifuna.
Awali, Orengo amekuwa akisisitiza kuwa bado yeye na wenzake ni wanachama wa ODM na wanapigania kukirejesha katika misingi yake ya awali.
Msemaji wa Linda Mwananchi Caroli Omondi amesema ODM imekufa kisiasa na kuwahimiza wanachama wake kuhamia Linda Mwananchi.
Pia amewataka viongozi wa upinzani akiwemo Kalonzo Musyoka, Rigathi Gachagua, Fred Matiang’i, Martha Karua, James Orengo na Edwin Sifuna kukubaliana kuhusu mgombea mmoja wa urais ili kumpa ushindani mkali Rais Ruto katika uchaguzi mkuu mwaka 2027.
Kwa upande wake, Sifuna amekuwa akisisitiza kuwa ushindi dhidi ya Rais Ruto utawezekana tu ikiwa upinzani utaweka kando maslahi binafsi na kuungana.
Tayari msemaji wa muungano wa upinzani Mukhisa Kituyi amesema timu ya Sifuna ni sehemu ya mazungumzo yanayoendelea ya kuunda muungano mpana wa upinzani.
Hata hivyo, wachambuzi wanasema bado haijulikani iwapo Sifuna atakuwa tayari kuacha azma yake ya urais ikiwa muungano huo utakubali mgombeaji mwingine.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Multimedia Profesa Gitile Naituli anaamini Sifuna ameibuka kama mmoja wa viongozi wakuu wa kizazi kipya cha upinzani na anaweza kubadilisha mwelekeo wa siasa za mwaka 2027.
Lakini wengine wanahoji iwapo eneo la Mlima Kenya litamuunga mkono mgombea ambaye hatoki eneo hilo, wakisema hilo linaweza kuwa changamoto kubwa kwa muungano wowote wa upinzani utakaoundwa kuelekea uchaguzi mkuu.