Habari

Linet Toto aagizwa kumlipa mfanyakazi wake Sh1 milioni

Na JOSEPH WANGUI May 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MAHAKAMA ya Ajira na Leba imeagiza Mwakilishi wa Wanawake wa Bomet, Linet Chepkorir Toto, kumlipa aliyekuwa mfanyakazi wake karibu Sh1 milioni kwa kufutwa kazi kinyume cha sheria huku kukiwa na madai kwamba mume wa mbunge huyo alichochea mfanyakazi huyo kufutwa kazi.

Mahakama iliamua kuwa Kipkirui Dominic Mutai hakutendewa haki alipofutwa kazi kama Naibu Meneja wa Kaunti katika afisi ya Bi Toto baada ya kuzuiwa kuingia katika afisi ya Bunge bila notisi, bila kushirikishwa katika kikao cha kinidhamu au barua rasmi ya kufutwa kazi.

Mahakama ilimzawadi Bw Mutai Sh990,110 pamoja na riba ya asilimia 14 kwa mwaka, ingawa alikuwa akiomba zaidi ya Sh2.8 milioni kama fidia.

Jaji alisema ushahidi wa Bw Mutai haukupingwa baada ya washtakiwa, ambao ni Bi Toto na afisi ya Mwakilishi wa Wanawake wa Bomet, kushindwa kuwasilisha stakabadhi za utetezi, taarifa za mashahidi au hoja zao mahakamani licha ya kupewa nafasi.

Bw Mutai aliambia mahakama kuwa aliajiriwa Oktoba 3, 2022 kwa kandarasi ya miaka mitano na mshahara wa Sh165,000 kwa mwezi.

Alisema matatizo yalianza Machi 2023 baada ya kupokea vitisho kutoka kwa mume wa Bi Toto kuhusu kuendelea kwake kufanya kazi katika afisi hiyo.

Kulingana na hukumu hiyo, Bw Mutai aliripoti vitisho hivyo katika Kituo cha Polisi cha Bomet chini ya nambari ya OB 19/13/04/2023.

Pia alieleza kuwa Aprili 20, 2023, mtu aliyetumwa na afisi ya mwakilishi huyo alichukua funguo za afisi kutoka kwake na kumzuia kuingia mahali pake pa kazi.

Mahakama ilisema mamlaka ya kuajiri au kufuta wafanyakazi ilikuwa ya afisi ya Mwakilishi wa Wanawake wala si watu binafsi.

Jaji alisema kufutwa kazi kwa Bw Mutai kulikiuka Sheria ya Ajira inayomtaka mwajiri kutoa sababu halali, notisi na nafasi ya kusikizwa kabla ya kumfuta mfanyakazi kazi.

Hata hivyo, mahakama ilikataa kumrudisha Bw Mutai kazini ikisema hatua hiyo haingewezekana katika mazingira yaliyopo.