Muda wa kusitishwa kwa mgomo wazidi kuyoyoma serikali bado ikisubiriwa kutoa suluhu
MUDA wa kusitishwa kwa mgomo wa sekta ya matatu kwa wiki moja unazidi kuyoyoma huku shinikizo zikiongezeka kwa serikali kutafuta suluhu ya kudumu kabla ya Jumanne ijayo ili kuzuia maandamano na kulemazwa kwa huduma za uchukuzi.
Serikali kupitia Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen, Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi pamoja na wadau wa sekta ya uchukuzi walikubaliana kusimamisha mgomo huo kwa muda wa siku saba huku mazungumzo zaidi yakitarajiwa kufanyika.
Hata hivyo, viongozi wa vyama mbalimbali za matatu (sacco)wameweka wazi kuwa hawatakubali chochote isipokuwa serikali ipunguze gharama ya mafuta, jambo ambalo wanasema limefanya biashara yao kuwa ngumu mno.
Akizungumza na Taifa Leo, mwenyekiti wa kitaifa wa Chama cha Wamiliki wa Matatu (MOA), Albert Karakacha, alisema wahudumu wa sekta hiyo hawatatishwa wala kushinikizwa kusitisha malalamishi yao.
“Malalamishi yetu lazima yashughulikiwe na Rais William Ruto mwenyewe kwa sababu hali imekuwa ngumu sana kwa sekta hii,” alisema Karakacha.
Miongoni mwa mambo wanayotaka ni kuanzishwa kwa mfumo huru wa bei za mafuta, kuvunjwa kwa Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA), kurejeshwa kwa ruzuku ya mafuta pamoja na kukomeshwa kwa hongo inayodaiwa na polisi wa trafiki barabarani.
Kwa mujibu wa Karakacha, kiwango cha chini wanachotaka ni punguzo la Sh46 kwa bei ya mafuta kama ilivyotangazwa awali na EPRA katika tangazo lake la kila mwezi la bei za mafuta.
Licha ya serikali kutangaza kupunguza bei ya dizeli kwa Sh10, sekta ya matatu ambayo hutegemea zaidi dizeli kuendesha magari yake imesema hatua hiyo haitoshi.
“Bado tunasubiri kuitwa kwa mkutano mwingine lakini kiwango chetu cha chini ni Sh46. Wametupatia Sh10 na sasa tunasukuma Sh36 iliyobaki,” alisema.
Alisema gharama kubwa ya mafuta imeathiri pakubwa shughuli za kila siku za wahudumu wa matatu huku pia bei ya vipuri vya magari ikiendelea kupanda.
Karakacha alisema fedha wanazotumia kila siku ni nyingi ikiwemo kulipa mikopo ya magari, ada za maegesho za kaunti, mishahara ya madereva na makanga pamoja na gharama za matengenezo ya magari.
“Sh46 tunayozungumzia ndizo zitasaidia kulipa mkopo wa magari, ada za maegesho ya kaunti, huduma za magari, mishahara ya madereva na makanga. Wakitupatia punguzo hilo mgomo utasitishwa kabisa,” alisema.
Aidha, alilalamikia ushuru unaotozwa na serikali za kaunti pamoja na serikali kuu akisema sekta hiyo imelemewa.
“Tunatumia pesa nyingi sana. Pia kuna ufisadi ambapo polisi wanachukua pesa kwa nguvu barabarani,” alisema.
Karakacha alisema kukutana moja kwa moja na Rais Ruto ndio matumaini yao ya mwisho kwani anaamini ndiye mwenye uwezo wa kutafuta fedha za kupunguza gharama ya mafuta.
“Tusipopata suluhu, gharama ya maisha itapanda zaidi na mwananchi wa kawaida ndiye ataumia. Tunapigania Wakenya wa kawaida kwa sababu hatutaki kuongeza nauli,” alisema.
Chama hicho pia kimetaka serikali kuanzisha magari mengi ya umeme ili kusaidia kupunguza kutegemea mafuta ghali.
Mwenyekiti wa kampuni ya Forward Traveler, Peter Mwangi, alisema serikali inapaswa kurejesha ruzuku ya mafuta ili kupunguza mzigo kwa Wakenya.
Pia alitaka serikali kuboresha hali ya barabara akisema wahudumu wa matatu hutumia fedha nyingi kutengeneza magari yanayoharibika kutokana na barabara mbovu.
Mwangi alikanusha madai yaliyoenea kwenye mitandao ya kijamii kuwa baadhi ya viongozi wa sekta ya matatu walihongwa na serikali kusitisha mgomo huo kwa muda.
“Hakuna aliyehongwa. Aliyetushawishi kusitisha mgomo ni Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja kwa sababu tumekuwa na ushirikiano mzuri na serikali ya kaunti,” alisema.
Aliongeza kuwa iwapo itabainika kuna yeyote aliyepokea hongo, sekta hiyo itafanya uchunguzi wake na kuchukua hatua kali.
Mwangi pia alipuuza madai kuwa baadhi ya viongozi wa matatu wanatumiwa kisiasa kuhujumu serikali ya sasa.
Kuhusu uwepo wa Dennis Itumbi katika mkutano wa viongozi wa matatu na serikali, Mwangi alisema wao wenyewe walimtafuta ili kusaidia kupanga mazungumzo hayo.
Jina la Itumbi limekuwa likijadiliwa sana nchini huku Wakenya wengi wakijiuliza nafasi yake katika mazungumzo ya sekta ya matatu ilhali yeye ni Mkuu wa Miradi Maalum ya Rais na Uratibu wa Uchumi wa Ubunifu.