Habari

SHA yaweka masharti makali kwa wanaotafuta matibabu ng’ambo

Na ANGELA OKETCH May 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

NI Mkenya mmoja pekee ambaye ameidhinishwa rasmi kupata matibabu nje ya nchi tangu kuanzishwa kwa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA) mnamo Oktoba 2024.

Idadi hiyo ndogo inaonyesha jinsi serikali ilivyoweka masharti makali kuhusu wagonjwa wanaoweza kufadhiliwa kwenda kutibiwa nje ya nchi, licha ya maelfu ya Wakenya kutafuta ruhusa ya kusafiri kila mwaka kwa matibabu ambayo hayapatikani nchini.

Kwa sasa, ni hospitali tisa pekee katika mataifa matatu ambazo zimeidhinishwa kushughulikia magonjwa 36 maalum yaliyotangazwa rasmi kufadhiliwa chini ya mpango huo.

Aidha, mgonjwa lazima apitie hatua tisa za kuidhinishwa kabla ya kupata barua ya dhamana ya matibabu.

Bila barua hiyo, SHA haitalipia matibabu yoyote nje ya nchi.

Waziri wa Afya, Aden Duale, alisema mgonjwa anayesafiri nje ya nchi bila idhini rasmi ya SHA atakuwa amefanya hivyo nje ya mfumo wa serikali.

“Bila idhini hiyo ya awali, SHA hairuhusiwi kubeba gharama za matibabu hayo,” alisema.

Hospitali zilizoidhinishwa ziko Uturuki, India na Saudi Arabia.

Nchini Uturuki, hospitali nne zilizo chini ya kundi la Acibadem zimeidhinishwa.

Hizi ni Acibadem Mehmet Ali Aydinlar University Atakent Hospital, Acibadem Maslak Hospital, Acibadem Altunizade Hospital na Acibadem Adana Hospital.

India imeidhinishiwa hospitali tatu ambazo ni Wockhardt Hospital, Apollo Cancer Centre na KIMS Hospital Enterprises Private Limited.

Saudi Arabia ina hospitali mbili zilizoidhinishwa ambazo ni Dr Soliman Fakeeh Hospital na King Faisal Specialist Hospital.

Mkurugenzi anayesimamia madai katika SHA, Golda Larissa, alisema mchakato wa kuidhinisha hospitali zaidi bado unaendelea.

Alisema hospitali hizo zimechaguliwa kwa sababu zina uwezo wa kufanya matibabu 36 ambayo hayapatikani kwa urahisi nchini Kenya.

Miongoni mwa magonjwa na matibabu yaliyotajwa ni upasuaji tata wa mifupa na viungo, ikiwemo kubadilisha vifundo vya mikono, vifundo vya miguu na sehemu za mifupa ya paja pamoja na matumizi ya mifupa ya kupandikiza.

SHA pia itafadhili matibabu tata ya watoto wachanga walio tumboni na matatizo ya ujauzito ambayo hayapatikani nchini.

Katika matibabu ya saratani, SHA itagharamia tiba inayobadilisha chembe za kinga za mwili wa mgonjwa ili kushambulia uvimbe wa saratani.

Pia kuna matibabu ambayo hupunguza madhara kwa tishu nyingine za mwili na tiba kwa aina fulani za uvimbe.

Matibabu mengine yanayofadhiliwa ni pamoja na upandikizaji wa ini, upandikizaji wa uboho, upandikizaji wa figo kwa watoto, upasuaji tata wa moyo kwa watoto, tiba maalum ya saratani ya macho kwa watoto na upandikizaji wa koo.

Hata hivyo, huduma nyingi ambazo Wakenya wengi huenda kutafuta nje ya nchi hazijajumuishwa katika orodha hiyo.

Bw Duale aliwaonya Wakenya dhidi ya kusafiri kwa matibabu ambayo yanaweza kutolewa nchini bila idhini ya SHA.

“Ukisafiri kwenda India kwa upasuaji wa nyonga, huduma hiyo haiko katika orodha ya matibabu 36 yaliyofadhiliwa. Huduma hiyo inaweza kutolewa nchini Kenya,” alisema.

Kubadilishwa kwa nyonga, upasuaji wa moyo, matibabu ya uti wa mgongo, upandikizaji wa figo kwa watu wazima na uchunguzi wa hali ya juu ni baadhi ya sababu kuu zinazowafanya Wakenya kusafiri kutafuta matibabu nje ya nchi, lakini hazifadhiliwi chini ya mpango huo.

Kwa wanachama wa kawaida wa SHA chini ya Hazina ya Bima ya Afya ya Jamii, kiwango cha juu cha fedha za matibabu nje ya nchi ni Sh500,000 pekee. Gharama yoyote inayozidi kiwango hicho italipwa na mgonjwa mwenyewe.

Kwa watumishi wa umma walio chini ya Hazina ya Matibabu ya Maafisa wa Umma, kiwango hicho ni Sh2.5 milioni, mara tano zaidi ya wanachama wa kawaida.

Serikali pia huwasaidia maafisa hao kupata tiketi za ndege za kwenda na kurudi pamoja na walezi wao.

Mfumo huo wa viwango viwili unamaanisha kuwa mtumishi wa umma na mfanyakazi wa sekta binafsi wenye ugonjwa sawa watapata ulinzi tofauti wa kifedha wanapotibiwa nje ya nchi.

Mchakato wa kuidhinishwa pia ni mrefu na wenye masharti mengi.

 

Hospitali ya Kenya inayomrejelea mgonjwa lazima itume nyaraka tano kwa SHA ikiwemo ripoti ya daktari mtaalamu, mpango wa matibabu kutoka hospitali ya nje ya nchi na makadirio ya gharama.

SHA hukagua nyaraka hizo kabla ya kumtaka mgonjwa kuwasilisha hati za utambulisho, pasipoti, visa na vyeti vya kuzaliwa kwa watoto.

Baada ya hapo mgonjwa hupewa barua za dhamana na SHA huandaa tiketi za ndege. Hospitali ya nje ya nchi pia hutakiwa kutoa taarifa za maendeleo ya mgonjwa kila wiki hadi matibabu yatakapokamilika.

Bw Duale alisema hatua hizo kali zinalenga kuhakikisha fedha za umma zinatumika kwa wagonjwa wanaohitaji matibabu ambayo hayawezi kupatikana nchini Kenya.