Jamvi La Siasa

Wanaositasita kuhamia upinzani wakisubiri dakika za mwisho wapewa onyo kali

Na BENSON MATHEKA May 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

UCHAGUZI mkuu wa 2027 ukikaribia viongozi wa kisiasa wanaosita kuhamia upinzani wakisubiri dakika za mwisho wameanza kupewa onyo kali.

Katika maeneo mbalimbali vinara wa upinzani sasa wanataka wanasiasa wachague mapema upande wanaounga mkono badala ya kusubiri kwanza mawimbi ya siasa yabadilike kabla kufanya maamuzi.

Gavana wa Trans-Nzoia George Natembeya ni mmoja wa viongozi waliotoa msimamo mkali zaidi.

Akizungumza katika kaunti yake Alhamisi, Natembeya alisema viongozi wa eneo la Magharibi ambao bado wako serikalini wanapaswa kubaki huko badala ya kuhamia upinzani dakika za mwisho kuelekea kindumbwendumbwe cha 2027.

Alisema hakuna sababu ya viongozi kuendelea “kula na serikali” wakati raia wanaumizwa na hali ngumu ya maisha, halafu wajitokeze baadaye wakitaka kuonekana kuwa watetezi wa wananchi.

“Mtu asikuambie anangoja mpaka mwaka ujao. Akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki. Sasa hivi wananchi wanaumia na wao wanakula,” alisema Natembeya huku akiwataka wakazi wa Trans-Nzoia kuwakataa viongozi watakaochelewa kujiunga na upinzani.

Kauli hiyo inaonyesha jinsi 2027 inazidi kuibuka kuwa mapambano ya uaminifu wa kisiasa na sio tu ushindani wa vyama.

Katika eneo la Gusii, aliyekuwa Seneta Maalum Gloria Orwoba naye alitoa onyo kama hilo wakati wa mazishi ya mamake Seneta Richard Onyonka huko Mosocho.

Orwoba alisema viongozi wa jamii ya Abagusii wana hadi Mei 25 kujiunga rasmi na upinzani na kumuunga mkono aliyekuwa Waziri wa Usalama Fred Matiang’i ambaye tayari ameidhinishwa na wazee wa jamii hiyo kama msemaji wao wa kisiasa.

Aliwataka viongozi wanaosubiri kuona upande utakaoonekana kushinda wajue kuwa watachelewa, na hivyo wananchi watawaadhibu debeni 2027.

Pia alimwonya Dkt Matiang’i dhidi ya kuwapokea viongozi watakaohama dakika za mwisho, akisema ni wale wamemuunga mkono tangu mwanzo ndio wanastahili kupewa nafasi ya kwanza.

Katika eneo la Mlima Kenya, aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua naye ametoa ujumbe kama huo kwa viongozi ambao bado hawajajiunga na chama chake cha Democracy for the Citizens Party (DCP).

Gachagua amesema mlango wa kujiunga na mrengo wake hautabaki wazi milele na kwamba viongozi wanaosubiri hadi uchaguzi ukaribie watajikuta nje ya mipango yake ya kisiasa.

Onyo hizi zinatolewa huku ikitabiri kwamba kutakuwa na wimbi la viongozi kutoroka serikali mara tu baada ya kusomwa kwa bajeti hapo mwezi Juni.