Habari

GenZ: Wabunge watetea raia kuhusu bajeti kubwa

Na DAVID MWERE May 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HUKU wabunge wakirejelea vikao vya bunge kesho baada ya mapumziko ya mwezi mmoja, viongozi hao wa kisiasa wameonya kuwa bajeti kubwa ya Sh4.8 trilioni itakuwa mzigo mkubwa kwa raia walipa-ushuru.
Kamati ya Bajeti inatarajiwa kuwasilisha ripoti yake kuhusu mapitio ya makadirio ya mapato ya serikali kwa mwaka wa kifedha wa 2026/27.
Kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Alego Usonga, Samuel Atandi, inatarajiwa kuwasilisha ripoti hiyo mnamo Juni 2, kisha kupisha majadiliano ya makadirio hayo.
Mswada wa Matumizi ya Fedha wa 2026 na Mswada wa Fedha wa 2026 unatarajiwa kujadiliwa na kamati mbalimbali kabla ya kusomwa kwa bajeti mwezi ujao.
Kamati ya bajeti imekuwa ikikutana na wadau mbalimbali na pia kuzunguka maeneo tofauti nchini kuwahamasisha wananchi kuhusu yaliyomo katika makadirio ya bajeti ya 2026/27.
Mswada wa Fedha wa 2026 pia utasomwa kwa mara ya kwanza, hatua itakayofungua njia kwa Kamati ya Fedha na Mipango ya Taifa kuanza kushirikisha umma kuhusu yaliyomo ndani yake.
Mswada huo tayari umeibua mjadala mkali kote nchini, huku viongozi wa Muungano wa Upinzani wakitishia kuongoza maandamano kuupinga jinsi ambavyo ilifanyika mnamo 2024.
Waziri wa Fedha John Mbadi, anatarajiwa kusoma bajeti ya mwaka huu mnamo Juni 11, 2026, kwa mujibu wa Kifungu cha 40 cha Sheria ya Usimamizi wa Fedha za Umma.
Tarehe hiyo imekubaliwa na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), kama ilivyo desturi ya kuratibu siku ya hotuba za bajeti kwa pamoja.
Wabunge pia watajadili marekebisho mbalimbali yaliyopendekezwa na Seneti kuhusu Mswada wa Ugavi wa Mapato wa 2026 na Mswada wa Ugavi wa Mapato kwa Kaunti wa 2026.
Mswada wa Ugavi wa Mapato unaeleza jinsi mapato yanayokusanywa na serikali ya kitaifa yatakavyogawanywa kati ya serikali ya kitaifa na serikali za kaunti.
Mswada huo ulipitishwa na Bunge la Kitaifa mnamo Machi 2026 na kuwasilishwa kwa Seneti ili kutathminiwa.
Hata hivyo, Seneti ilifanya marekebisho kadhaa kwenye mswada huo, na hivyo italazimu Bunge la Kitaifa kuujadili tena kwa ajili ya kuridhia au kukataa mabadiliko hayo.
Aliyekuwa Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Kenya (KRA), Humphrey Wattanga, pia atafahamu hatima yake Jumanne kuhusu iwapo uteuzi wake wa kuwa Balozi Mkuu wa Kenya mjini Ottawa, Canada, utaidhinishwa.
Kamati ya Ulinzi, Ujasusi na Mahusiano ya Kigeni inayoongozwa na Mbunge wa Belgut, Nelson Koech, ilimhoji Bw Wattanga mnamo Mei 14, 2026, na inatarajiwa kuwasilisha ripoti yake kuhusu iwapo anafaa kuiwakilisha Kenya nchini Canada.
 Bunge pia litafanya uamuzi kuhusu ombi lililowasilishwa na Waziri wa Mazingira, Mabadiliko ya Tabianchi na Misitu, Dkt Deborah Barasa, kuhusu kuondolewa kwa hadhi ya kisheria (de-gazettement) kwa sehemu maalum za misitu minne ya umma pamoja na kushughulikia madai yanayohusiana na maeneo hayo.
Misitu inayohusika ni pamoja na Msitu wa Nandi Kusinikatika eneo la Chepkumia, Msitu wa Turbo katika eneo la Manzini, Msitu wa Mount Elgon katika eneo la Chepkyuk, na Msitu wa Kakamega katika maeneo ya Shiru/Shaviringa.