Usalama wa Rais Ruto wamulikwa ‘akivamiwa’ tena akiwa jukwaani
USALAMA wa Rais William Ruto kwa mara nyingine umemulikwa baada ya mwanamume kumvamia jukwaani akihutubu Ganze, Kaunti ya Kilifi.
Rais alikuwa akihutubu katika ibada ya shukrani kwa Katibu wa Wizara ya Vijana, Bw Fikirini Jacobs, wakati kijana mmoja alipokimbia hadi jukwaani akiwa ameshika kitabu kilichoonekana kama Biblia.
Kwa muda mfupi, Rais Ruto alionekana kuwa tayari kumsikiliza kijana huyo alipokaribia na kumsogelea, akimpa sikio.
Hata hivyo, maafisa wa usalama walimkimbilia na kumvuta kutoka jukwaani.
Ilibidi Rais awazuilie maafisa hao kumshambulia, ambapo alisikika akiwaomba wamuache huku akimsaidia kusimama.
Baadaye aliagiza apelekwe kuketi katika eneo la wageni maalumu (VIP).
“Huyo kijana hana shida nafikiri amejifunza kutoka kwa Fikirini Jacobs, kwamba nafasi ikipatikana asiipoteze. Huyo kijana wachana naye tutamshughulikia baadaye ni kijana mzuri anajitafutia bahati yake,” Rais alisema baada ya tukio hilo lililokatiza kwa muda hafla hiyo.
Hivi majuzi, mnamo Februari, mwanamume alikimbia kuelekea kwa Rais wakati akihutubia vijana katika hafla ya mpango wa kitaifa wa kuwezesha vijana (NYOTA) Wajir kabla ya kuzuiwa.
Mapema mwezi huohuo, kijana mwingine alikimbilia jukwaani wakati wa hafla kama hiyo mjini Mombasa. Mnamo Mei 2025, kiatu kilirushwa kuelekea Rais Ruto wakati wa mkutano wa hadhara huko Migori.