Wakenya hawatakula maneno matupu ya ‘hasla’ na ‘dynasty’, Uhuru amponda Ruto
RAIS Mstaafu Uhuru Kenyatta jana alimshambulia mrithi wake Rais William Ruto na kuwahimiza Wakenya kuhakikisha hachaguliwi tena 2027.
Bw Kenyatta pia aliwakashifu baadhi ya viongozi wa Kenya Kwanza kwa kukumbatia siasa za ukabila.
Bw Kenyatta alisema badala ya kushughulikia matatizo ya kiuchumi yanayowaathiri wananchi, utawala wa Kenya Kwanza umeamua kuendeleza mchezo wa kulaumiana na siasa za kikabila.
Katika ukosoaji wake wa hivi punde ambao unaonekana kama maandalizi ya pambano jingine la kisiasa mnamo 2027, Bw Kenyatta aliwakumbusha Wakenya jinsi alivyowaonya mnamo 2022 dhidi ya kuchagua utawala wa sasa.
Aliwataka wapige kura kwa hekima katika uchaguzi mkuu ujao.
Bw Kenyatta alimuunga mkono marehemu kiongozi wa ODM Raila Odinga chini ya muungano wa Azimio la Umoja mnamo 2022 lakini wakabwagwa na Rais Ruto ambaye wakati huo alikuwa naibu rais.
Hata baada ya kustaafu amekuwa akijihusisha na siasa za Jubilee na ashatangaza kuwa katika uchaguzi mkuu wa 2027, atamuunga mkono aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani, Dkt Fred Matiang’i.
Dkt Matiang’i ni kati ya viongozi walio katika Muungano wa Upinzani ambao pia una Rigathi Gachagua wa DCP, Kalonzo Musyoka (Wiper), Martha Karua (PLP), Justin Muturi (DCP) na Eugene Wamalwa wa DAP-K.
Akizungumza na wajumbe na wagombea wa Jubilee kutoka Kaunti ya Kiambu, Bw Kenyatta pia alifunguka kuhusu mzozo wa uongozi ndani ya chama hicho ambao aliulaumu kwa nguvu za nje.
Wachanganuzi wa masuala ya kisiasa, wanaamini kuwa mvutano mpya kati ya Bw Kenyatta na Rais Ruto unaweza kuhusishwa na mapambano ya kudhibiti eneo lenye wapigakura wengi Mlima Kenya kuelekea uchaguzi wa 2027.
Dkt Ruto alimng’oa Bw Kenyatta kama kigogo wa siasa kutoka eneo hilo katika uchaguzi wa 2022 kwa kushinda viti vingi kupitia chama chake cha UDA.
Bw Kenyatta naye anaonekana kuwa na azma ya kurejesha ushawishi wake 2027.
Kuendelea kushiriki siasa pia kunaonekana kama njia ya kulinda maslahi makubwa ya biashara ya familia ya Kenyatta.
Baadhi ya vongozi wa Kenya Kwanza wamekuwa wakimlaumu Bw Kenyatta kwa madai ya kutatiza utawala wa Rais Ruto kwa kufadhili maandamano na mikutano ya kisiasa ya upinzani.
“Unapoanza kulaumu watu na kujaribu kuwagawa, hilo linasaidiaje nchi hii kusonga mbele? Masuala yanayowaathiri Wakenya hayana kabila, rangi wala dini,” akasema Bw Kenyatta.
“Wakenya wamekasirika kwa sababu ya gharama ya juu ya maisha. Wanalalamikia bei ya juu ya mafuta, wasikilizeni Wakenya badala ya kuhamisha lawama. Ikiwa mnahitaji msaada, tupigieni simu na kwa pamoja tutapata suluhu,” akaongeza.
Rais huyo mstaafu alisema ukabila unaoenezwa na baadhi ya viongozi wa UDA unaweza kuiingiza nchi katika ghasia za kisiasa kama zilizoshuhudiwa mwaka 2007.
“Tumeanza kuona wengine wakieneza siasa za kikabila zinazogawa watu. Hawana aibu kusema mambo hayo. Wanatoa matamshi hayo mbele ya viongozi wa nchi yetu, na hakuna anayewazuia,” akasema.
Alionekana kumrejelea Katibu Mkuu wa UDA Hassan Omar ambaye amekosolewa vikali kutokana na matamshi aliyotoa mbele ya Rais Ruto, ambayo yalionekana kulenga jamii moja nchini.
Bw Kenyatta pia alirejelea simulizi ya “hasla na dynasty” ambayo Rais Ruto aliitumia kuingia mamlakani.
Katika kampeni zake za 2022, Rais Ruto alijizolea uungwaji mkono wa wananchi wengi wa mapato ya chini kwa kuahidi kupunguza gharama ya maisha na kuunda nafasi za ajira kwa vijana wasio na kazi.
“Mmenufaika vipi na siasa za dynasty au hasla? Mlipotoshwa na nilikuwa nimewaonya. Niko hapa kuwakumbusha tena, msije mkasema sikuwaonya. Wakileta pesa, kuleni, lakini siku ya kupiga kura, pigeni kura kwa anayefaa,” Bw Kenyatta akawaambia wajumbe hao Jubilee.
“Watu wangu, nimewafungulia moyo wangu na nawasihi muwe na hekima ya kuwachagua viongozi na si wanasiasa.”
Mkutano wa jana pia ulihudhuriwa na viongozi wakuu wa Jubilee akiwemo Dkt Matiang’i, Naibu Kiongozi wa chama Jeremiah Kioni, na Katibu Mkuu Moitalel Ole Kenta.
Kiambu ni mojawapo ya kaunti muhimu zinazotarajiwa kuangaziwa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027 huku serikali na upinzani zikijaribu kuvutia wapigakura.