Bajeti 2026: Wabunge waogopa ‘GenZ’, wafuta baadhi ya vipengele kupunguza hasira
WABUNGE nchini sasa wanaonekana kuchukua tahadhari kubwa wanapoandaa Bajeti ya Mwaka wa Kifedha 2026, huku Mswada wa Fedha wa 2026 ukizua mjadala mpana kuhusu kile kilichoondolewa na kile kipya kilichoingizwa katika mfumo wa kodi nchini.
Mswada huo unaonekana kubeba maamuzi makubwa ya sera, lakini pia umeacha baadhi ya mapendekezo yaliyokuwa yameibua hasira ya wananchi katika mswada wa 2024, uliosababisha maandamano makubwa ya vijana na hatimaye marekebisho ya haraka ya baadhi ya vifungu vyake.
Miongoni mwa yaliyotolewa kwenye mswada mpya ni VAT ya asilimia 16 kwenye mkate, ushuru wa kila mwaka wa asilimia 2.5 kwa magari, na VAT kwenye usafirishaji wa miwa kutoka mashambani kwenda viwandani.
Vilevile, kipengele kilichokuwa kikiruhusu Mamlaka ya Mapato Kenya (KRA) kupata taarifa za miamala ya M-Pesa bila amri ya mahakama hakijarejeshwa katika muundo wake wa awali.
Serikali pia imeongeza misamaha ya VAT kwa bidhaa za nishati safi na huduma za afya. Bidhaa zilizonufaika na msamaha huo ni pamoja na baiskeli za umeme, pikipiki na mabasi ya umeme, pamoja na betri za sola .
Mashine za kusafisha damu pia zimeongezwa kwenye orodha ya bidhaa zisizo na VAT, sambamba na malighafi za uzalishaji wa chakula cha mifugo na dawa.
Hata hivyo, kile kinachoibua mjadala mpya ni upanuzi wa wigo wa ushuru kwenye uchumi wa kidijitali.
Mswada huo umeweka wajibu wa ushuru kwa watumiaji wa sarafu za kidijitali, wafanyabiashara wa majukwaa ya mtandaoni, waundaji wa maudhui na miamala ya kadi za malipo.
Hatua hiyo inajiri wakati ukosefu wa ajira kwa vijana Kenya bado uko juu, na wengi wamejikita katika kazi za mtandaoni kama njia mbadala ya kipato kutokana na uhaba wa ajira rasmi.
Wanauchumi wanasema kwamba, kutoza kodi sekta ya kidijitali si jambo geni, lakini mafanikio yake yatategemea muundo wa utekelezaji na uwezo wa serikali kuhakikisha uzingatiaji bila kuathiri ukuaji wa sekta hiyo changa.
Serikali haijatoa ufafanuzi wa kina jinsi hatua hizo mpya zitakavyoathiri makundi tofauti ya kipato nchini.

Mswada huo unatarajiwa kupitia hatua ya pili na tatu bungeni mnamo Juni kabla ya kuanza kutumika rasmi tarehe Julai 1, baada ya kutiwa saini na Rais kuwa sheria.
Huku mjadala ukiendelea, baadhi ya wabunge wanasemekana kuwa kupata presha kubwa kutokana na kumbukumbu za mswada wa awali uliosababisha mvutano mkali kati ya serikali na wananchi.
Kwa vijana wanaojihusisha na kazi za kidijitali, wasiwasi mkubwa sasa ni kama mapato yao yasiyo na uhakika yataweza kubeba mzigo mpya wa ushuru unaopendekezwa katika mswada huo.
Miongoni mwa mapendekezo mapya ni ushuru wa bidhaa wa asilimia 25 kwa kila simu ya mkononi inayowashwa nchini Kenya, iwe imeagizwa kutoka nje au imetengenezwa ndani ya nchi. Ushuru huo utatozwa wakati kifaa kinapoanza kutumika.
Kwa simu inayouzwa Sh15,000, mtumiaji atalazimika kulipa ziada ya Sh3,750, huku simu ya Sh10,000 ikiongezeka kwa Sh2,500.Wachambuzi wanasema hatua hiyo inaweza kuongeza gharama ya kumiliki vifaa muhimu vya kazi kwa vijana wengi wanaotegemea simu zao kujipatia kipato katika sekta ya kidijitali.
Baadhi ya vijana wanaojihusisha na kazi za mtandaoni wanasema gharama ya vifaa tayari ni kubwa, na ongezeko la ushuru litafanya uwekezaji wa kidijitali kuwa mgumu zaidi.

Mswada huo pia umeweka wazi kuwa ongezeko hilo la ushuru halihusiani na VAT, ambayo simu tayari zimepata msamaha, bali ni kodi tofauti ya ushuru wa bidhaa. Hii ina maana kuwa msamaha wa VAT hauondoi athari za ushuru wa bidhaa.
Tofauti na mapendekezo ya 2024 yaliyolenga zaidi vifaa vinavyoagizwa kutoka nje, hatua ya 2026 inahusisha simu zote bila kujali asili yake, jambo ambalo limeibua mjadala mpya kuhusu athari zake kwa sekta ya utengenezaji wa ndani na uchumi wa kidijitali.
Serikali haijatoa tathmini rasmi ya athari za hatua hiyo kwa watumiaji wala makadirio ya mapato yanayotarajiwa kukusanywa kupitia ushuru huo.
Mswada huo ni wa tatu wa fedha kuletwa tangu mwaka 2024, kipindi kilichoshuhudia maandamano makubwa yaliyolazimisha baadhi ya vifungu vya awali kuondolewa au kurekebishwa.
Wataalamu wa ushuru wanasema kuwa mabadiliko ya sasa yanaonyesha juhudi za serikali kupanua wigo wa mapato bila kurejesha moja kwa moja mapendekezo yaliyozua mvutano hapo awali.