Kafyu Lamu: Polisi wakaa ngumu kuhusu safari za usiku licha ya agizo la mahakama
POLISI kaunti ya Lamu wanasema hawatarejesha safari za usiku eneo hilo hadi watakapopokea amri kutoka kwa Waziri wa Usalama wa Ndani, Kipchumba Murkomen na Inspekta-Jenerali wa Polisi, Douglas Kanja.
Alhamisi wiki iliyopita Mahakama Kuu ya Garsen, kaunti ya Tana River ilitoa amri iliyopiga breki marufuku ya safari za usiku kwenye barabara ya Lamu-Witu-Garsen ambayo imekuwa ikitekelezwa kwa miaka tisa, hali iliyotoa afueni kubwa kwa wakazi.
Polisi hata hivyo wamekaidi kutekeleza agizo hilo.
Ni hali iliyopelekea mabasi, malori na magari mengine yanayopita katika barabara hiyo kufunga makutano ya barabara Minjila Jumanne kama mbinu mojawapo ya watumiaji wa barabara hiyo kupinga vizuizi vya kusafiri saa kumi na mbili jioni hadi saa moja asubuhi.
Hali hiyo ililazimisha magari na abiria wanaotoka pande zote za Lamu, Garsen, Garissa, Malindi na Mombasa kkutatizika kwani hakukuwa na njia ya kupita kuendelea na safari zao.
Akizungumza na Taifa Leo Jumatano, Kamanda wa Polisi kaunti ya Lamu, Bw Shadrack Ruto aliitaja hatua ya watumiaji kufunga barabara kuwa hatia.
Alishikilia kuwa walinda usalama walioko mashinani Lamu hawajapokea maelekezo yoyote kutoka kwa wakuu wao ambao ndio waliopokezwa agizo la mahakama moja kwa moja.
“Sisi hutekeleza maagizo tunayopewa na wakuu wetu. Tunalofahamu kwa sasa ni kwamba marufuku ya usiku Lamu ipo. Waziri Murkomen na Inspekta-Jenerali Douglas Kanja ndio waliopokezwa amri ya korti na sio sisi wa mashinani. Tutaruhusu usafiri wa usiku kurejelewa punde tukipokea maagizo kutoka kwa wakuu wetu,” akasema Bw Ruto.
Alisisitiza juhudi zinazotekelezwa na walinda usalama Lamu kuhakikisha usalama wa raia wanotumia barabara unadhibitiwa.
Alikiri kuimarika kwa usalama kwenye barabara ya Lamu-Witu-Garsen na kaunti nzima miaka ya hivi karibuni.
“Hatujashuhudia visa vya ugaidi, ikiwemo magari ya walinda usalama na raia kushambuliwa. Yote ni kutokana na juhudi za maafisa wetu. Ila suala la kuondolewa kwa marufuku ya safari za usiku na vizuizi barabarani linafaa kujadiliwa kwa undani zaidi kabla ya maamuzi yoyote kuchukuliwa,” akasema Bw Ruto.
Kauli yake inajiri wakati ambapo wanaharakati wa haki za binadamu na jamii kaunti ya Lamu tayari wamejitokeza kushinikiza safari za usiku zirejelewe.
Wakizungumza na wanahabari Jumatano, wanaharakati walitisha kushiriki maandamano makubwa zaidi hivi karibuni na kusitisha shughuli zote za usafiri na biashara hadi pale safari za usiku zitakaporejelewa.
“Watii amri ya korti kwa kuruhusu safari za usiku. Tunawapa makataa ya siku tatu la sivyo tutaandamana na kukwamisha shughuli zote,” akasema Bw Mohamed Skanda, mwanaharakati.