Mkasa wa moto waua wanafunzi 16 Utumishi Girls Gilgil, Waziri Ogamba athibitisha
WANAFUNZI 16 wamethibitishwa kufariki katika mkasa wa moto uliotokea katika shule ya Utumishi Girls iliyoko Gilgil, Kaunti ya Nakuru.
Ripoti ya polisi inasema kwamba moto huo uliripotiwa saa saba za usiku katika bweni la wanafunzi 220 wa Gredi ya 10, Kidato cha Tatu na Kidato cha Nne.
Inasema juhudi za kuzima moto zilizoongozwa na zimamoto wa Naivasha, KDF, Idara ya Misitu na NYS zilisaidia kukabili moto huo ingawa tayari maafa yalikuwa yametokea huku idadi isiyojulikana ya waliojeruhiwa wakikimbizwa katika hospitali mbali mbali.
Viongozi wa ngazi za juu serikali akiwemo Waziri wa Usalama Kipchumba Murkomen, Waziri wa Elimu Julius Ogamba, Katibu wa Elimu Julius Bitok, Mkuu wa DCI Mohamed Amin, Naibu Mkuu wa Polisi Eliud Lagat na Kamati ya Bunge kuhusu Elimu wamefika shuleni humo kutathmini hali.
Akizungumza na wanahabari, Waziri Ogamba alisema shughuli ya kutambua walioangamia inaendelea huku akitoa nambari ambayo wazazi wanaweza kupiga kutafuta maelezo na kupata ushauri nasaha.
“Tunaomba wazazi kutumia nambari 1199 kuripoti haswa iwapo ni wale walioondoka na watoto wao walipowasili mapema. Nambari hiyo pia itatumika kutoa ushauri nasaha,” akasema Bw Ogamba.
Wakati huo huo, waziri huyo alitangaza kufunga shule hiyo kwa muda kuruhusu uchunguzi kufanywa kuhusu kilichosababisha moto katika bweni hilo la Meline Waithera Block.