MKASA: Imebainika kuwa walimu walifahamu mpango wa kuchoma shule ya Utumishi
SERIKALI Ijumaa Mei 29, 2026 ilisema walimu wawili wa Shule ya Sekondari ya Utumishi Girls Senior School walikuwa na taarifa za mapema kuhusu uwezekano wa fujo lakini hawakuchukua hatua kabla ya tukio la Alhamisi usiku ambalo bweni lilichomwa.
Waziri wa Elimu Julius Ogamba alisema walimu hao walikuwa wamepata tahadhari mapema kutoka kwa baadhi ya wanafunzi wa Kidato cha Tatu waliokuwa na taarifa za mpango wa kuchoma moto shule.
“Hata hivyo, walimu hao hawakuchukua hatua kuzuia tukio hilo, licha ya kuwa walikuwa wamearifiwa mapema,” alisema Bw Ogamba.
Aliongeza kuwa Tume ya Huduma ya Walimu (TSC) imejulishwa kuhusu matokeo hayo na hatua za kinidhamu zitachukuliwa dhidi ya mkuu wa shule pamoja na walimu waliohusika.
“TSC imefahamishwa matokeo haya( ya uchunguzi) na inachukua hatua za haraka za kinidhamu dhidi ya Mkuu wa Shule kwa kushindwa kuhakikisha Mwongozo wa Usalama wa Shule na Kanuni za Elimu ya Msingi. Walimu waliokosa kuchukua hatua licha ya kuarifiwa kuhusu mpango huo watachukuliwa hatua za kinidhamu,” alisema.
Ufichuzi huo ulijiri wakati uchunguzi wa awali wa DCI ulionyesha kuwa moto uliosababisha vifo vya wanafunzi 16 na kujeruhi wengine 79 ulikuwa wa makusudi na uliopangwa.
DCI ilithibitisha imekamata wanafunzi wanane wanaoshukiwa kuhusika na mpango huo.