Habari

Mpango wa Amerika kujenga kituo cha Ebola Kenya yazimwa

Na JOSEPH WANGUI May 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu imesitisha kwa muda mpango wa serikali wa kuanzisha au kuwezesha kituo chochote cha kutenga au kutibu Ebola chini ya makubaliano ya Kenya na Amerika, saa chache baada ya Washington kutangaza mpango wa kutoa mamilioni kukabiliana na ugonjwa huo.

Mahakama pia imezuia mpango wa kuwapokea waathiriwa wa Ebola nchini chini ya makubaliano hayo yenye utata.

Amri hizo za muda zilitolewa baada ya shirika la kutetea haki za kiraia la Katiba Institute kushtaki serikali kuhusu uamuzi wa kuanzisha kituo cha kutenga wagonjwa wa Ebola kaunti ya Laikipia kushughulikia raia wa Amerika wanaoambukizwa Ebola.

Katiba Institute ilieleza kuwa makubaliano hayo yalifikiwa bila ushirikishaji wa wananchi, bila usimamizi wa Bunge na bila kufichuliwa kwa masharti yake kwa umma.

Maafisa wa afya wa Amerika tayari wako nchini Kenya wakijiandaa kuanzisha kituo hicho kitakachotumika kuwahifadhi raia wa Amerika wanaoshukiwa au wanaoambukizwa Ebola katika ukanda huu.

Mahakama ilitoa amri hizo saa chache baada ya Washington kuthibitisha mazungumzo ya ngazi ya juu kati ya Rais William Ruto na Waziri wa Masuala ya Kigeni wa Amerika Marco Rubio kuhusu maandalizi ya Ebola, ufadhili na uratibu kati ya mataifa hayo mawili.

Katika taarifa ya Wizara ya Masuala ya Kigeni ya Amerika kupitia msemaji Tommy Pigott, utawala wa Rais Donald Trump ulielezwa kuwa viongozi hao walijadili kuimarisha mfumo wa afya wa Kenya, kuhakikisha upatikanaji wa vifaa muhimu vya matibabu na kuratibu majibu ya mlipuko wa Ebola unaoendelea katika ukanda huu.

Amerika ilitangaza pia mpango wa kutoa Sh1.7 bilioni kwa Kenya kwa ajili ya maandalizi ya Ebola, sambamba na msaada wa Sh14.4 bilioni kukabiliana na ugonjwa huo katika kanda hii.

Hata hivyo, Mahakama Kuu Nairobi ilitoa amri za muda zinazozuia serikali kuanzisha, kuendesha au kuruhusu kituo chochote cha Ebola hadi kesi isikilizwe kikamilifu.

Katiba Institute ilisema mpango huo unaibua masuala mazito ya afya ya umma, utawala bora na uhuru wa taifa.

Mahakama ilikubali kesi hiyo kuwa ya dharura na kusema kuwa maslahi ya umma yanahitaji hatua za haraka za kusitisha utekelezaji wa mpango huo hadi isikilizwe.

Serikali imeagizwa kujibu hoja hizo ndani ya muda uliowekwa kabla ya kesi kusikilizwa tena Juni 2.

Katika hoja zake, Katiba Institute ilisema Kenya haina miundombinu ya kutosha kushughulikia Ebola, ikibainisha kuwa virusi hivyo vinahitaji maabara za kiwango cha juu cha Biosafety Level Four, ilhali Kenya ina BSL-1 hadi BSL-3 pekee, ikiwa ni tatu tu za kiwango cha BSL-3 nchini kote.

Shirika hilo pia lilihoji iwapo taifa linaweza kweli kudhibiti mlipuko endapo utatokea kutokana na ukosefu wa uwezo wa kitaalamu na miundombinu.

Pia lilishutumu serikali kwa kushindwa kufichua masharti ya makubaliano hayo, tathmini za mazingira, tafiti za usalama wa viumbe hatari na taratibu za matibabu.

Katiba Institute ilisema makubaliano yoyote yanayohusu afya ya umma na usalama wa taifa yanapaswa kupitiwa na Bunge chini ya Katiba na sheria ya mikataba ya kimataifa.

Mahakama imeagiza Katiba Institute kuwasilisha stakabadhi za kesi kwa washtakiwa ndani ya saa 24, huku washtakiwa wakitakiwa kujibu ndani ya saa 48 baada ya kupokea stakabadhi hizo.