OneTam: Sifuna aidhinishwa kuwa kigogo wa Mulembe
SENETA wa Kakameg,a Boni Khalwale amemuidhinisha Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna kama kigogo wa siasa za Jamii ya Mulembe na kusema sasa ana baraka za kuongoza jamii hiyo kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Akiongea katika Kaunti ya Bungoma wikendi, Dkt Khalwale alidai kuwa Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi na Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula, wameshindwa kuonyesha uongozi mwema na sasa wakati umetimia Bw Sifuna achukue usukani.
“Bw Sifuna una jukumu kubwa na tumia heshima ambayo tumekupa kusaka mamlaka na maendeleo kwa wakazi wa eneo hili,” akasema Dkt Khalwale.
Kauli yake iliungwa mkono na Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya ambaye alisema kama jamii wako tayari kuunga mkono Bw Sifuna katika siasa za kitaifa kwa sababu utawala wa Kenya Kwanza haujawafaa wakazi wa eneo hilo.
“Viongozi kutoka eneo hili huwa wamejaa wivu na wanafurahi kiongozi akiteswa. Wale ambao wanafanya kazi na Rais Ruto, hatutakubali mjiunge na sisi. Kazi yangu ni kuwaunganisha Waluhya na kama ni Sifuna, sote tutakuwa nyuma yake,” akasema Bw Natembeya.
Katibu huyo mkuu wa ODM pia alipata uungwaji mkono kutoka kwa Mbunge wa Bumula Wanami Wambako na mwanasiasa mkongwe Dkt Noah Wekesa.
“Katika meza hiyo ya mazungumzo ambapo watu wanazungumzia masuala ya kitaifa, Bw Sifuna lazima awe hapo,” akasema Dkt Wekesa kwenye hafla ya mazishi ya marehemu Patrick Wamangati wikendi.