Dondoo

Mganga atimua mbio demu wa zamani alipomjia kama mteja

Na KALUME KAZUNGU June 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

PALAKUMI, Kilifi:

MGANGA tajika kijijini hapa hivi majuzi aligutuka na kuchomoka kutoka kilingeni kwake baada ya kugundua mteja aliyefika kutafuta usaidizi wa kummaliza ex wake alikuwa mpenziwe wa zamani.

Demu husika aliachana na mwanamume huyo miaka saba iliyopita kabla ya jamaa kujitosa kwenye shughuli za uganga.

Demu alikuwa ameudhiwa na jamaa huyo kwa kukatiza uhusiano wao ghafla.Alimwapia kwamba siku moja angetumia njia zozote zile ilmuradi amuue.

Hivi majuzi, demu alifika kilingeni bila kutambua aliyemtafuta kumhudumia ex wake anayetaka kumwangamiza.

Akiwa kilingeni, demu hakumtambua mganga kutokana na kujichorachora kwake huku akivalia magwanda yaliyoziba sehemu nyingi za uso wake.

Mganga pia hakumtambua demu haraka kwani alikuwa amevaa buibui na kujiziba usoni kwa ninja.

Mganga alipouliza ufafanuzi zaidi kumhusu ex wa demu ili amalizane naye aligutuka kusikia jina lake kamili na hata familia anayotoka ikitajwa.

Kufumba na kufumbua mganga aliruka kutoka kilingeni na kutimka.