Makala

Polisi aliyekufa baada ya gwaride Madaraka Dei alipata mshtuko wa moyo

Na KEVIN ODIT June 2nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

AFISA wa polisi wa Kitengo cha General Service Unit (GSU) ambaye alianguka na kufariki muda mfupi baada ya kushiriki gwaride la sikukuu ya Madaraka wakati wa sherehe za kitaifa zilizohudhuriwa na Rais William Ruto katika Kaunti ya Wajir, alifariki kutokana na mshtuko wa moyo, kulingana na ripoti ya polisi.

Konstebo Hassan Moyo alianguka muda mfupi baada ya gwaride la polisi katika Uwanja wa Wajir mnamo Jumatatu asubuhi katika hafla hiyo ya kitaifa iliyohudhuriwa na viongozi na wakazi.

“Afisa huyo alianguka mara tu baada ya gwaride katika Uwanja wa Wajir majira ya saa tatu na dakika tano asubuhi,” sehemu ya ripoti ya polisi ilisema.

Alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kaunti ya Wajir ambapo alitangazwa kufariki dunia saa nne asubuhi.

Ripoti hiyo ilionyesha kuwa, afisa huyo alifariki kutokana na ‘myocardial infarction’, inayojulikana zaidi kama mshtuko wa moyo.

Kakake mkubwa, Bw Ali Moyo, alisema jamaa wake wanaoishi Kwale walishtushwa na kifo hicho kwa sababu Hassan hakuwahi kuugua maradhi yoyote yaliyofahamika.

“Hata mimi ni jambo linanitatiza kwa sababu toka azaliwe hajawahi kuwa na ugonjwa wowote unaomsumbua. Alikuwa mzima kabisa,” alisema.

“Alikosa fursa ya kujiunga na jeshi na baadaye akaingia GSU ambapo alifanya kazi kwa bidii. Hili limekuwa pigo kubwa kwa familia yote,” akaongeza.

Kulingana na familia yake, marehemu alijiunga na taasisi ya mafunzo ya vikosi vya usalama mwaka wa 2017 kabla ya kuhitimu na kujiunga na kikosi maalum cha RECCE cha GSU mwaka wa 2018.

Alihudumu awali katika Kaunti za Garissa na Turkana kabla ya kuhamishiwa Nairobi chini ya kikosi cha RECCE.

Afisa huyo, ambaye alikuwa mwanafunzi wa zamani wa Shule ya Upili ya Kwale na alimaliza shule ya upili mwaka wa 2011, ameacha mke na watoto wawili wadogo wenye umri wa miaka mitano na mitatu.

Familia hiyo imeiomba serikali kuwasaidia watoto hao kimaisha.

Binamu yake, Bw Salim Moyo, ambaye ni mwanahabari anayeishi Mombasa, alisema familia bado inatatizika kukubali kifo hicho cha ghafla, akimtaja marehemu kama mtu mwenye nguvu na afya njema kabla ya kifo chake.

“Mipango imewekwa ili ndugu yetu marehemu azikwe kwa mujibu wa taratibu za Kiislamu katika nyumba yetu ya familia kijijini Magaoni, Golini, Kaunti ya Kwale,” alisema Salim.

Babake marehemu, Juma Ali Moyo, alitarajiwa kuwasili kuuona mwili huo kabla ya kusafirishwa hadi Kaunti ya Kwale kwa mazishi baadaye Jumanne.

Habari za kifo chake zilienea mitandaoni baada ya Mbunge Mwakilishi wa Wanawake wa Kwale Fatuma Masito kutuma ujumbe wa rambirambi katika ukurasa wake wa mitandao ya kijamii.

Sherehe za kuadhimisha sikukuu ya Madaraka kitaifa mwaka huu zilifanyika katika Kaunti ya Wajir zikiongozwa na Rais Ruto.

Hafla hiyo iliwaleta pamoja viongozi wa kitaifa, maafisa wa usalama na mamia ya wakazi kusherehekea miaka 62 tangu Kenya ijitawale.

Sherehe hizo zilijumuisha gwaride la vikosi vya usalama, burudani za kitamaduni na hotuba kuhusu maendeleo, usalama na umoja wa kitaifa.