Walimu hatarini serikali ikikosa kutenga Sh5.3bn za bima muhimu
WALIMU zaidi ya 400,000 walioajiriwa na Tume ya Huduma ya Walimu (TSC) wako hatarini baada ya serikali kukosa kutenga Sh5.3 bilioni za bima ya maisha, ajali na majeraha ya kazini waliyokuwa wakinufaika nayo hapo awali.
Kamati ya Elimu ya Bunge la Kitaifa imefichua kuwa bajeti ya mwaka wa kifedha 2026/2027, haina fedha za kugharamia bima hizo kwa walimu.
Kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Tinderet Julius Melly, ilisema hali hiyo imewaacha walimu katika mazingira magumu hasa baada ya kuhamishwa kutoka mpango wa bima binafsi uliokuwa ukisimamiwa na kampuni ya Minet chini ya NHIF hadi mfumo wa Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA).
“Hakuna fedha zilizotengwa kwa bima ya maisha, ajali binafsi na fidia ya majeraha ya kazini kwa walimu. Ni muhimu TSC ipatiwe rasilimali za kutosha kuhakikisha walimu wanapata huduma hizi kwa sababu zinahusu ustawi wao,” ilisema kamati hiyo.
Ripoti hiyo imeibua maswali kuhusu iwapo walimu walipata huduma bora baada ya kuhamishwa kwa SHA mnamo Desemba 2025.
Wakati huo huo, imebainika kuwa walimu wanakatwa fedha mara mbili kila mwezi kugharamia Hazina ya Bima ya Afya ya Jamii (SHIF) na Hazina ya Huduma za Afya kwa Maafisa wa Umma (POMSF), zote zikisimamiwa na SHA.
Kamati hiyo ilibaini pia kuwa serikali bado ina deni la Sh4.4 bilioni kwa kampuni ya Minet baada ya kandarasi ya bima ya walimu kukamilika.
Kati ya deni la awali la Sh7.4 bilioni, serikali ililipa Sh3 bilioni kupitia bajeti ya ziada mwaka huu wa kifedha, na kuacha salio la Sh4.4 bilioni ambalo halijajumuishwa katika makadirio ya bajeti ya TSC ya mwaka wa 2026/2027.
Kwa mujibu wa kamati hiyo, TSC iliokoa takriban Sh4 bilioni baada ya kuhamisha walimu kutoka mpango wa bima binafsi hadi SHA.
Fedha hizo, ilisema, zinaweza kutumika kurejesha bima ya maisha na ajali kwa walimu.
Mbunge wa Kitutu Chache South, Bw Anthony Kibagendi, alionya kuwa walimu wanaweza kulazimika kutumia fedha zao binafsi kulipia matibabu hasa wale wanaougua magonjwa sugu.