Siasa

Wimbi la Sifuna latikisa vigogo wa kisiasa wa miaka mingi Magharibi

Na CECIL ODONGO June 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MABADILIKO makubwa ya kisiasa yanaendelea kushuhudiwa katika eneo la Magharibi mwa Kenya huku Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna akijitokeza kama sauti mpya inayotikisa vigogo wa muda mrefu wa siasa za eneo hilo.

Katika mazishi na mikutano ya hadhara, viongozi wengi sasa hulazimika kueleza wazi iwapo wanamuunga mkono Bw Sifuna na vuguvugu lake la “Linda Mwananchi” ili kupata umakini wa wananchi.

Kauli ya kuunga mkono seneta huyo huibua shangwe kutoka kwa umma, huku maoni tofauti yakipokelewa kwa tahadhari.

Kuibuka kwa Bw Sifuna kumeleta changamoto kwa viongozi wa zamani wa eneo hilo akiwemo Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi na Spika wa Bunge la Kitaifa Moses Wetang’ula, ambao wamekuwa wakitawala siasa za Magharibi tangu kifo cha aliyekuwa Makamu wa Rais Kijana Wamalwa mwaka 2003.

Umaarufu wa Bw Sifuna umeongezeka si Magharibi pekee bali pia kitaifa, hasa miongoni mwa vijana wa kizazi cha Gen Z.

Kauli yake maarufu ya “Mimi ndiye Sifuna” imevutia wengi, huku uwezo wake wa kujieleza ukimfanya kuwa mmoja wa wanasiasa wanaofuatiliwa zaidi nchini.

Nguvu zake zilidhihirika mwishoni mwa wiki iliyopita wakati wa mazishi ya aliyekuwa mbunge mteule na mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Waluhya, Mzee Patrick Wangamati, katika eneo la Kabuchai, Bungoma.

Katika mazishi hayo, viongozi wa upinzani pamoja na mwanasiasa mkongwe Noah Wekesa, walimtangaza Bw Sifuna kama kiongozi mpya anayechipuka katika eneo hilo na kuwakosoa Mabw Mudavadi na Wetang’ula kwa kile walichodai ni kushindwa kushughulikia changamoto za muda mrefu zinazowakabili wakazi wa Magharibi.

Ingawa Bw Sifuna hajatangaza iwapo atawania urais mwaka 2027 au kutetea kiti chake cha useneta wa Nairobi, baadhi ya viongozi tayari wanamuona kama sura mpya ya kisiasa inayoweza kubadilisha mwelekeo wa eneo hilo.

Hata hivyo, Gavana wa Bungoma, Bw Kenneth Lusaka, amepuuzilia mbali madai kuwa Bw Sifuna yuko tayari kuwania urais, akisema bado hana uzoefu wa kutosha wala rasilimali za kuendesha kampeni ya kitaifa.

“Sisi hatuna chuki. Waluhya tunataka kutoa rais wa Kenya, lakini lazima tupange vizuri. Sifuna ana kipaji lakini wakati wake bado,” alisema Bw Lusaka.

Bw Lusaka, ambaye ni mshirika wa karibu wa Bw Wetang’ula na mratibu wa kampeni za Rais William Ruto katika eneo la Magharibi, alisisitiza kuwa jamii hiyo inapaswa kumuunga mkono Rais Ruto hadi mwaka 2032 kabla ya kutafuta urais.

Lakini viongozi wa upinzani wana mtazamo tofauti. Seneta wa Vihiga, Bw Godfrey Osotsi, alisema Bw Sifuna ameweza kujijengea taswira ya kitaifa na kukubalika katika jamii mbalimbali tofauti na siasa za kikabila zilizotawala eneo hilo kwa muda mrefu.

“Kinachohitajika si umri au muda ambao mtu amekuwa katika siasa, bali aina ya uongozi anaotoa,” alisema Bw Osotsi.
Seneta wa Kakamega, Dkt Boni Khalwale, pia anaamini mustakabali wa jamii ya Mulembe uko mikononi mwa Bw Sifuna.

“Waluhya si wajinga tena. Tunahitaji viongozi watakaotuletea maendeleo na nguvu kisiasa,” alisema Dkt Khalwale katika mkutano Bungoma.

Naye Gavana wa Trans Nzoia, Bw George Natembeya, alisema viongozi wa Magharibi wanaounga mkono serikali wamekuwa wakiwataka wananchi kusubiri hadi mwaka 2032 ilhali maendeleo yanayohitajika hayajafika.

“Kama ni Sifuna atakayeunganisha Waluhya, tutasimama nyuma yake,” alisema Bw Natembeya.

Hata ndani ya upinzani, umaarufu wa Bw Sifuna umeanza kubadilisha mwelekeo wa kisiasa.

Kiongozi wa Wiper, Bw Kalonzo Musyoka, tayari ameonyesha yuko tayari kufanya kazi naye katika juhudi za kumuondoa Rais Ruto mamlakani mwaka 2027.

Utafiti wa shirika la Trends and Insights for Africa (TIFA) mwezi uliopita, ulionyesha kuwa tiketi ya Kalonzo-Sifuna ni miongoni mwa zinazoungwa mkono na wafuasi wa upinzani.

Wakati huo huo, mikutano ya “Linda Mwananchi” iliyofanyika Busia, Vihiga na Kakamega imevutia umati mkubwa, jambo linaloonyesha kuwa Bw Sifuna anazidi kujijengea ushawishi katika eneo ambalo kwa muda mrefu limeongozwa na wanasiasa waliokomaa.

Huku uchaguzi wa 2027 ukikaribia, kuibuka kwa Bw Sifuna kunaonekana kubadilisha mizani ya siasa za Magharibi na kuibua mjadala mpya kuhusu nani atakuwa sauti kuu ya jamii ya Mulembe katika siasa za kitaifa.