Serikali yazidi kubanwa kuhusu Ebola licha ya kujitetea inarudisha mkono kwa Amerika
SERIKALI ya Rais William Ruto inaendelea kuwekewa presha baada ya Mahakama Kuu kuamuru Wizara ya Afya kufichua maelezo kamili ya mpango unaohusisha kuanzishwa kwa kituo cha karantini na matibabu ya Ebola kwa raia wa Amerika nchini Kenya.
Hatua hii imezua mjadala mkali wa kitaifa kuhusu usalama wa afya ya umma, uwazi na mamlaka ya Katiba huku maandamano yakifanywa Nairobi na Nanyuki kupinga makubaliano hayo.
Mahakama jana ilielekeza Waziri wa Afya, Aden Duale, kutoa ndani ya siku saba stakabadhi zote za makubaliano, ikiwemo mkataba wowote, mazungumzo au memoranda ya maelewano kati ya Kenya na Amerika kuhusu mpango huo.
Aidha, mahakama imeagiza serikali kuelezea iwapo Bunge, mamlaka za kaunti au idara zilihusishwa kabla ya maamuzi hayo kufikiwa.
Katika uamuzi huo, mahakama pia imesisitiza kuwa serikali lazima itoe taarifa zote za tathmini ya athari kwa afya ya umma, mazingira, usalama wa viumbe hai pamoja na taratibu za utunzaji, karantini na matibabu ya watu wanaoweza kuwa wameambukizwa au kuathiriwa na Ebola.
Kesi hiyo imevutia hisia kali za wananchi, ambapo zaidi ya watu 350 walihudhuria kwa njia ya mtandao, ishara ya kiwango cha wasiwasi ulioibuliwa na mpango huo wa kujengwa kwa kituo hicho katika kambi ya kijeshi ya Laikipia.
Mahakama pia imezuia serikali kuendelea na ujenzi au kuanzisha kituo chochote cha karantini au matibabu ya Ebola nchini, huku ikiunganisha kesi ya Shirika la Katiba Institute na ile ya Chama cha Wanasheria Nchini (LSK).
Mashirika mengine kama Tume ya Haki za Binadamu (KHRC) na Serikali ya Kaunti ya Laikipia yameruhusiwa kujiunga kama wahusika katika kesi hiyo.
Kesi hiyo itatajwa tena Juni 23 ili kuthibitisha utekelezaji wa amri za mahakama.
Katiba Institute inasema serikali inajaribu kugeuza Kenya kuwa “kituo cha karantini cha mataifa ya kigeni” bila ruhusa ya wananchi wala uwazi wa mikataba hiyo.
LSK pia imehoji kuwa mpango huo haukupitishwa na Bunge wala kufanyiwa tathmini ya mazingira na afya, jambo linalokiuka Katiba.
Wakati huo huo, maandamano yamezuka katika maeneo mbalimbali, yakipinga kituo hicho.
Jijini Nairobi, wanaharakati waliandamana hadi Wizara ya Afya, Afya House, wakitaka mradi huo usitishwe mara moja.
“Tutapinga kila hatua ya serikali ya kuleta kituo cha Ebola nchini Kenya,” alisema mwanaharakati Ojilo Odhiambo, akisisitiza kuwa wananchi hawakushirikishwa.
Kaunti ya Laikipia, wakazi wa Nanyuki pia waliandamana wakipinga kituo hicho kinachopendekezwa katika kambi ya kijeshi ya Laikipia Air Base.
Waandamanaji walisema hakuna mashauriano ya umma yaliyofanyika kabla ya uamuzi huo kufikiwa.
“Hatukukubali kabisa kituo cha Ebola kiwe karibu na makazi yetu. Hili ni jambo hatari,” alisema mkazi mmoja, John Mwangi.
Sekta ya utalii Nanyuki pia imeathirika baada ya wageni kufuta safari zao kufuatia taarifa za mpango huo.
Wawekezaji wanasema wamepata hasara kubwa kufuatia hofu ya wageni.
Baadhi ya viongozi wa kisiasa wamesema serikali inapaswa kusikiliza wananchi kabla ya kuendelea na mradi huo.
Gavana wa Embu, Cecily Mbarire, amesema Kenya haipaswi kuharakisha ujenzi wa kituo hicho bila mashauriano ya kutosha.
Serikali inasisitiza kuwa Kenya inabaki kuwa mshirika muhimu wa kimataifa katika masuala ya afya na kwamba, maandalizi ya magonjwa ya mlipuko ni sehemu ya usalama wa kitaifa.
Rais Ruto ametangaza kuwa alitoa idhini ya kujengwa kituo hicho kufuatia ombi la mwenzake wa Amerika, Donald Trump aliyesema Amerika imekuwa ikisaidia Kenya na nchi inapaswa kurudisha mkono.
Hata hivyo, shinikizo za kisiasa, kisheria na kijamii zinaendelea kuongezeka, huku wananchi wakitaka uwazi kamili kuhusu mustakabali wa mradi huo wenye utata mkubwa.