Habari za Kaunti

Kibarua kwa Achani wapinzani wakiungana dhidi yake

Na WINNIE ATIENO June 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SIASA za ugavana Kwale zimechukua mkondo mpya baada ya wapinzani wakuu wa Gavana Fatuma Achani, kutangaza mpango wa kuungana na kuunga mkono mmoja wao 2027.

Aliyekuwa Katibu wa Wizara ya Kilimo, Prof Hamadi Boga, na Mwenyekiti wa Chuo cha Bandari Maritime Academy, Bw Mangale Lungazi, wamepanga kuungana katika harakati za kuwania kiti hicho.

Wawili hao, waliowania ugavana katika uchaguzi mkuu wa 2022 na kuibuka wa pili na wa tatu mtawalia, sasa wameamua kuweka tofauti zao kando na kushirikiana kwa lengo la kumshinda Bi Achani katika uchaguzi mkuu ujao.

Aliyekuwa Waziri wa Uchukuzi Bw Chirau Mwakwere, ambaye pia alikuwa mgombeaji, alisema atawaunga mkono wawili hao katika azma yao.

“Tuko pamoja na nia yetu ni kuunganisha watu wa Kwale. Mmoja wetu atakuwa gavana na mwingine naibu gavana kwa sababu hatuwezi kuwa magavana sote wawili kwa wakati mmoja,” akasema Prof Boga.

Alieleza kuwa, mpango wao ni kuunda muungano utakaoleta uongozi wa ushirikiano kama ule wa marehemu Rais Mwai Kibaki na mwenzake Bw Raila Odinga wakati wa serikali mesto.

Ushirikiano aina hiyo pia ulishuhudiwa kati ya serikali na upinzani wakati wa utawala wa rais mstaafu Uhuru Kenyatta, na hivi sasa katika uongozi wa Rais William Ruto, ambao unatarajiwa kuendelea hadi katika uchaguzi ujao.

Aliongeza kuwa yeyote atakayeteuliwa kupeperusha bendera ya muungano huo atakubaliwa na mwenzake kwa lengo kuu la kuwahudumia wakazi wa Kwale na kuwaondoa katika changamoto za kiuchumi.

Kwa upande wake, Bw Lungazi ambaye alikuwa mwanachama wa PAA alisema serikali ya sasa ya kaunti imeshindwa kutekeleza miradi ya maendeleo, hasa katika sekta za afya na kilimo.

Chama cha PAA kilitangaza hakitakuwa na wagombeaji katika uchaguzi ujao, bali kitaunga mkono serikali.

“Hakuna mipango madhubuti ya kuhifadhi maji, ndiyo maana bado tunakabiliwa na changamoto za maji. Miaka 14 baada ya ugatuzi, hospitali zetu bado ziko katika hali mbaya,” alisema Bw Lungazi.

Bi Achani alipuuzilia mbali muungano huo akisema wawili hao wameshikwa na wasiwasi wa uchaguzi mkuu ujao.

“Watu wameanza kushikwa na wasiwasi na sasa wanashirikiana ili kupata kura kwa sababu hawana imani wanaweza kuwahudumia wakazi wote wa Kwale. Mimi ninaweza kwenda sehemu yoyote kwa sababu nawafanyia kazi wananchi wote bila kuangalia kabila,” alisema Bi Achani wakati wa hafla ya kuapishwa kwa makamishna wapya wa Bodi ya Ajira ya Kaunti ya Kwale.

Kauli zao zinajiri wiki chache baada ya Waziri wa Madini na Uchumi wa Baharini, Bw Hassan Joho, kuapa kumpigia debe Bi Achani ili amalize mihula yake miwili ya uongozi.

Awali, kulikuwa na uhasama kati ya Bi Achani na Bw Joho lakini kauli ya Waziri huyo iliashiria walitatua tofauti zao.

Bi Achani alianza safari yake ya kisiasa mwaka 2013 alipoteuliwa kuwa Naibu Gavana wa aliyekuwa gavana wa kwanza wa Kwale, Bw Salim Mvurya, ambapo walihudumu pamoja kwa miaka 10.

Baadaye aliwania ugavana mwaka 2022 na kushinda katika kinyang’anyiro kikali dhidi ya Prof Boga wa ODM.

Prof Boga na Bw Lungazi walisisitiza kuwa wameamua kuungana kwa sababu serikali ya Bi Achani imeshindwa kutimiza matarajio ya wakazi wa Kwale.