Habari za Kitaifa

Wavulana 10 wa Alliance wanaoshukiwa kuchoma stoo ‘waliwasiliana na watu wa nje’

Na KEVIN CHERUIYOT, MERCY SIMIYU June 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WANAFUNZI 10 wa Shule ya Upili ya Alliance, Kikuyu, wamekamatwa kuhusiana na moto ulioteketeza stoo ya kuhifadhi godoro Jumatano usiku, huku uchunguzi wa awali ukionyesha kuwa huenda walikuwa na mawasiliano na wanafunzi wa shule nyingine kupanga vurugu hizo.

Maafisa wa shule walifichua habari hiyo wakati wa mkutano wa dharura uliofanyika jana kati ya wazazi na uongozi wa shule, ambapo ilibainika kuwa baadhi ya wanafunzi walitaka kusitisha masomo na kurejea nyumbani kabla ya muda rasmi uliopangwa.

Mwenyekiti wa Bodi ya Usimamizi wa shule hiyo, Sam Ncheeri, alisema hali ya wasiwasi iliongezeka shuleni humo kufuatia visa vya hivi majuzi vya moto katika shule mbalimbali za bweni nchini.

Alisema kamera za usalama zilirekodi wanafunzi wawili wakichoma ghala hilo, huku wengine wanane wakihusishwa na kupanga njama hiyo.

“Baadhi yao walikuwa wakisema wanataka kuondoka shuleni na kurejea nyumbani. Mmoja wa waliokamatwa alikuwa amewahi kueleza kuwa hakuwa na furaha kuendelea kusomea hapa,” alisema Ncheeri.

Kutokana na tukio hilo, shule ilifungwa kwa muda na wazazi kuagizwa kuwachukua watoto wao huku uchunguzi ukiendelea.

Ncheeri aliwataka wazazi kutumia muda huo kuzungumza na watoto wao kuhusu tabia na changamoto wanazokumbana nazo.

“Mnaporudi nyumbani na watoto wenu, sikilizeni wanachopitia. Ikiwa kuna ambaye hataki kuendelea kusomea hapa, basi suala hilo lizungumzwe kwa utaratibu,” alisema.

Mkurugenzi wa Elimu wa Kanda ya Kati Sabina Aroni, alisema kuna uwezekano wanafunzi hao walishawishiwa na wenzao kutoka shule nyingine.

“Tuliamua kuwa wanafunzi warejee nyumbani ili kupunguza wasiwasi miongoni mwao na wazazi wao. Alliance imekuwa mojawapo ya shule zenye nidhamu bora nchini na tunatarajia hali hiyo irejeshwe,” alisema.

Mkuu wa shule hiyo, David Kamau, alisema matatizo yalianza wakati baadhi ya wanafunzi walipozima taa katika madarasa manne jioni, jambo lililozua taharuki na kuwafanya walimu kuchunguza kilichokuwa kinaendelea.

Baadhi ya wazazi walishukuru uongozi wa shule kwa kuwafahamisha mapema kabla hali haijaharibika zaidi, huku wengine wakitaka wanafunzi waliokamatwa wasiruhusiwe kurejea shuleni hadi uchunguzi na hatua za kinidhamu zikamilike.

Wakati huo huo, serikali imesisitiza kuwa shule hazitafungwa mapema licha ya kuongezeka kwa visa vya vurugu na uchomaji wa mali katika taasisi za elimu.

Akizungumza katika hafla ya kutoa zawadi katika Shule ya Kenya High, Katibu wa Elimu ya Msingi, Profesa Julius Bitok, alisema hakuna sababu ya kubadilisha kalenda ya masomo kwa sababu chini ya asilimia moja ya shule nchini ndizo zimeathiriwa na vurugu.

“Shule zitaendelea na masomo hadi mapumziko ya katikati ya muhula yaliyopangwa kuanza Juni 24. Hakuna sababu ya kufunga shule mapema kwa sababu ya visa vichache vilivyoripotiwa,” alisema.

Aliongeza kuwa wizara imewaagiza wakuu wa shule kuwa macho dhidi ya dalili za vurugu, akisema mara nyingi migogoro hiyo huhusishwa na mitihani na shinikizo la masomo.

Tukio la Alliance limetokea siku chache baada ya moto katika Shule ya Utumishi Academy kuwaua wanafunzi 16, jambo ambalo limezidisha mjadala kuhusu usalama wa wanafunzi katika shule za bweni nchini.