Habari

Gachagua kujua hatima yake leo

Na MOSES NYAMORI na KEVIN CHERUIYOT June 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

ALIYEKUWA Naibu wa Rais, Rigathi Gachagua, amesema yuko tayari kupokea uamuzi wa Mahakama Kuu kuhusu kesi ya kutimuliwa kwake madarakani.
Kiongozi huyo wa DCP, kwa upande mwingine, ameapa kupambana hadi mwisho kwa kukata rufaa iwapo hukumu haitamridhisha.
Uamuzi unaotarajiwa kutolewa leo na jopo la majaji watatu una athari kubwa kisiasa kwa Bw Gachagua pamoja na wanasiasa wengine wakuu akiwemo Rais William Ruto, taifa linapoelekea katika uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2027.
Mbali na Rais Ruto na Bw Gachagua, matokeo ya kesi hiyo yanaweza pia kuathiri matarajio ya kisiasa ya kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka na naibu kiongozi wa Jubilee, Dkt Fred Matiang’i, ambao wanamezea mate urais.
Iwapo mahakama itabatilisha kuondolewa kwake madarakani, huo utakuwa ushindi mkubwa kwa Bw Gachagua.
Uamuzi huo unaweza kufungua nafasi ya kulipwa fidia na marupurupu ya mamilioni ya pesa.
Bw Gachagua aliondolewa madarakani baada ya kuhudumu kwa miezi 24 pekee. Mshahara wake wa jumla ulikuwa karibu Sh1.2 milioni kwa mwezi, ukijumuisha mshahara halisi wa Sh736,313, marupurupu ya nyumba ya Sh300,000 na yale ya usafiri pamoja na marupurupu mengine.
Sheria ya Kustaafu kwa Naibu Rais na Maafisa Wengine wa Serikali ya 2015 pia inampa pensheni ya kila mwezi inayolingana na asilimia 80 ya mshahara wake.
Katika nyaraka zake za mahakamani, anataka kulipwa mshahara na marupurupu yote ya muhula kamili wa miaka mitano pamoja na pensheni.
Muhimu zaidi, ushindi mahakamani utamruhusu kuwania nafasi yoyote ya kisiasa, ikiwemo urais katika uchaguzi wa 2027. Pia utampa uhai wa kisiasa ambao ni muhimu kwa azma yake ya nafasi yoyote ya uongozi.
Wadadisi wa kisiasa wanaamini kuwa mazingira ya kisiasa nchini yanaweza kubadilika pakubwa iwapo atashinda kesi hiyo na kuamua kuwania urais. Kwanza, atapata fursa ya kukabiliana moja kwa moja na Rais Ruto. Hata hivyo, kwa upande wa upinzani, hatua hiyo inaweza kuwavuruga na kusababisha wajipange upya.
Baadhi ya viongozi wa upinzani wanamwona Bw Gachagua kama mtu mwenye uwezo wa kuamua mshindi wa uchaguzi. Ikiwa ataamua kuwania urais, hali hiyo inaweza kusababisha mabadiliko makubwa ya kisiasa na baadhi ya viongozi wa upinzani kubadili misimamo au miungano yao.
Mwanzoni, Bw Gachagua alionekana kutokuwa na hamu ya kuwania urais kutokana na mjadala kuhusu iwapo alikuwa na sifa za kugombea baada ya kutimuliwa madarakani au la. Ingawa hivyo, amekuwa akionekana kama anayemuunga mkono Bw Musyoka kuwa mgombea wa urais wa upinzani.
Iwapo mahakama itatupilia mbali ombi lake, Bw Gachagua amesema atakata rufaa dhidi ya uamuzi huo.
Akizungumza jana baada ya kuhudhuria ibada katika kanisa la PCEA, Karen, Nairobi, Bw Gachagua alieleza imani yake kuwa atashinda mahakamani.
“Nina imani kwamba mahakama yetu ni huru, haina upendeleo na itamtendea haki Rigathi Gachagua na mamilioni ya wafuasi wake kote nchini. Ikiwa uamuzi utaenda upande mwingine, bado ni sawa. Tutakuwa na fursa ya kuenda katika Mahakama ya Rufaa na kufuata njia za kisheria zilizowekwa na Katiba,” akasema.
Bw Gachagua, ambaye ameonyesha nia ya kumng’oa Rais Ruto katika uchaguzi wa 2027, alisisitiza kuwa aliondolewa madarakani kinyume cha sheria na Katiba.
“Niliondolewa afisini kinyume cha sheria na Katiba na kesi imesikilizwa na hukumu itatolewa kesho (leo). Tuko tayari kwa matokeo yoyote. Ikiwa majaji wataamua kwamba tulitendewa visivyo na kubatilisha mchakato wa kunitimua, tutamshukuru Mungu na pia tutashukuru kwamba kuna mfumo wa haki unaofanya kazi nchini Kenya,” akasema.
Kiongozi huyo wa DCP aliwataka wafuasi wake kudumisha amani kabla na baada ya uamuzi huo.
“Nilipoondolewa madarakani, waliohusika walikuwa wakicheka wakisema Rigathi ameondolewa na wafuasi wake hawasemi chochote. Ni mimi niliwaambia wasiseme chochote. Niliwaomba wadhibiti hasira zao kwa sababu sisi ni watu wa amani na tunaamini katika kutatua mambo kwa njia ya amani.”
“Ningependa kuwaomba wafuasi wetu ambao wamekasirishwa na yanayoendelea nchini wasizue vurugu au kuenda kinyume cha sheria. Niliwaomba wadhibiti hasira zao lakini wazihifadhi. Mwaka ujao watapata fursa ya kuonyesha hisia zao kupitia kura.”
Majaji Anthony Mrima, Eric Ogolla na Frida Mugambi wanatarajiwa kutoa uamuzi huo. Bw Gachagua amesema Rais Ruto anaweza kuondolewa madarakani tu ikiwa upinzani utadumisha umoja na viongozi wake wawe tayari kuweka kando maslahi yao binafsi. Hata hivyo, amesisitiza kuwa yeye ndiye mwenye nafasi bora zaidi ya kumzima Rais Ruto.
“Tukishinda tutamshukuru Mungu, na tusiposhinda bado tutamshukuru kwa rehema na ukuu wake,” akasema .
Mchanganuzi wa siasa, Dismas Mokua, anaonya kuwa iwapo Bw Gachagua ataruhusiwa kuwania urais, hatua hiyo inaweza kumnufaisha Rais Ruto. Anasema wagombea wengi wa upinzani watagawa kura za wanaopinga serikali na kurahisisha ushindi wa Rais Ruto.