Dimba

UDAKU: Mwanahabari asema hali halali sababu ya penzi la Pep Guardiola

Na SINDA MATIKO June 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MWANAHABARI Natalie Pike aliwasaidia mashabiki wa Manchester City kumuaga kocha Pep Guardiola kwa kuchapisha mtandaoni ujumbe uliosema: “Nakupenda Pep.”

Wawili hao walianza kuwa marafiki wa karibu kwenye kituo cha runinga cha Man-City.

Natalie, ambaye ni mwanamitindo wa zamani wa jarida la FHM, alifanya mahojiano ya mwisho na Guardiola ugani Etihad mnamo Mei 24 mwaka huu na kupigwa picha naye siku iliyofuata katika dhifa ya kumwambia kocha huyo kwaheri uwanjani Co-op Live.

Baadaye, Natalie ambaye pia anafanya kazi katika BBC Radio Five, talkSPORT, DAZN na Race Day TV, alichapisha video kwenye Instagram ikimuonyesha akikumbatiana na Guardiola huku wakipapasana na kubusiana peupe.

Kwenye ujumbe unaorejelea mafanikio yake katika utangazaji wa soka, kipusa huyo aliandika kwenye Instagram: “Nakupenda sana Pep wangu. Nitakustahi milele. Umechochea kukua kwangu kitaaluma na umenikomaza zaidi kimahaba.”

Pep, 55, yuko katika harakati za kukamilisha talaka kati yake na Cristina Serra ambaye ameishi naye katika ndoa kwa zaidi ya miaka 30. Kocha huyo amekuwa akipigwa picha za mara kwa mara na Natalie huku mwanahabari huyo akiwa mwepesi wa kuzipakia kwenye mitandao ya kijamii.

Chanzo kimoja katika klabu hiyo kilisema: “Natalie alikuwa na mazoea ya kufanyia Pep na wachezaji wa Man-City mahojiano mengi. Hapo ndipo urafiki wao ulianzia na sasa wamependana. Tutarajie Natalie ajaze nafasi ambayo imeachwa na Cristina katika familia ya Pep.”

Natalie, 43, alianza kushabikia Man-City mnamo 2011, miaka mitano kabla ya Guardiola ambaye ni baba wa watoto watatu kuajiriwa na klabu hiyo. Inaaminika kuwa Natalie alianza kumtambalia Guardiola kimapenzi mnamo 2024 baada ya mkufunzi huyo kubwagana na Cristina, 53.

Wandani wa Guardiola wamesema uhusiano wake na mkewe umehama kutoka kuwa wa “kirafiki na wa kimahaba” na kuwa wa “mazungumzo ya mara chache na mawasiliano mabovu.”

Wanahabari wazoefu wa Uhispania – Laura Fa na Lorena Vazquez – ambao walikuwa wa kwanza kufichua mgogoro kati ya Guardiola na mkewe, wamesisitiza kwamba hakuna uwezekano wowote wa ndoa ya wawili hao kusalia imara.

Tofauti na Cristina ambaye tayari amevua pete yake ya ndoa, Guardiola angali na pete yake kidoleni na amekuwa akisafiri sana Uhispania ili kujaribu “kuokoa ndoa yao”.